2013-06-29 07:24:27

Yaliyojiri katika maisha na utume wa Papa Francisko!


Miezi kadhaa imekwisha yoyoma tangu Papa Francisko alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki. Watu wengi wameguswa na maneno, matendo na ushuhuda wake wa kazi za kichungaji, jambo ambalo limewaacha wengi wakiwa wameshikwa na bumbuwazi, kwani kwao, matukio haya yote ni kama kielelezo cha ari na mwamko mpya wa Injili ya Kristo, inayojikita katika Uinjilishaji mpya. RealAudioMP3

Waamini wanakumbushwa kwamba, Yesu anaendelea kuliongoza Kanisa lake kwa njia ya Roho Mtakatifu na kwamba, watu wengi ambao wamekata tamaa kutokana na magumu na shida mbali mbali za maisha, wanasubiri kusikia ujumbe wa matumaini ukitangazwa mioyoni mwao.

Haya ndiyo yanayojitokeza mjini Vatican, kwa kuona umati mkubwa wa watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wakienda kumsikiliza, kumwangalia na kukutana na Baba Mtakatifu Francisko ambaye kwa miezi ya hivi karibuni amekuwa ni gumzo la vyombo vya habari kitaifa na kimataifa!

Ni maneno ya Monsinyo Piero Coda, Mwanataalimungu na Jalim kutoka Chuo Kikuu cha Sophia anayechambua kwa kina na mapana matukio mbali mbali yanayoendelea kujiri katika maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko. Ni kiongozi ambaye amepokelewa vyema katika medani mbali mbali za maisha na hivyo kuwasha moto wa matumaini kwa wale waliokuwa wamekata na kujikatia tamaa ya maisha. Amewagusa waamini na wasioamini kutokana na maneno na matendo yake ya kila siku.

Baba Mtakatifu Francisko ameonesha unyenyekevu wa Mama Kanisa unaogusa mioyo ya watu na kuacha chapa ya kudumu, kama vile Yesu mwenyewe alivyotenda alipokuwa hapa duniani. Amewagusa walimwengu waliokuwa wameelemewa na kumezwa na malimwengu, lakini bado wana kiu ya kutaka kumfahamu Mungu kutoka katika undani kabisa wa mioyo yao! Huu ni mwamko mpya wa Uinjilishaji Mpya, ambao ni mapambazuko ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko anayefanya hija pamoja na Familia ya Mungu sehemu mbali mbali za dunia, ni sawa na mkate unaomegwa kwa ajili ya wengi! Ni kiongozi anayeshirikisha ujumbe na changamoto za Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani, chemchemi mpya ya imani na matumaini kwa wengi!

Baba Mtakatifu Francisko anatambua dhamana yake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, anayepaswa kushirikiana kwa karibu zaidi na Maaskofu mahalia waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia, kama sehemu ya utekelezaji wa dhamana na majukumu yake kama Kiongozi mkuu wa Kanisa Katoliki. Anaendelea kukazia umuhimu wa Sinodi za Maaskofu kama kielelezo cha umoja na mshikamano wa Kanisa katika kupembua, kupanga na kutekeleza mikakati ya shughuli za kichungaji pamoja na kuendelea kusoma alama za nyakati.

Moyo wake wa unyenyekevu umemwezesha katika miezi ya uongozi wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro kupendwa na kukubalika na wengi. Watu bado wanakumbuka ile siku ya kwanza alipoinamisha kichwa chake, akiomba sala kutoka kwa waamini; wazo ambalo ameliendeleza kwa nyakati tofauti tofauti anapokutana na watu. Hili ni tukio la kihistoria litakalobaki katika historia kwa kipindi cha miaka mingi.

Monsinyo Piero Coda anasema, mchakato wa Uinjilishaji Mpya umepata chimbuko lake katika Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican; ukavaliwa njuga na Papa Paulo wa sita, aliyelihamasisha Kanisa kuuinjilisha ulimwengu; dhana iliyofanyiwa kazi kwa kina na mapana na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili aliyezunguka sehemu mbali mbali za dunia, akiwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumfungulia Kristo malango ya maisha yao bila woga.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, akawaandaa waamini kwa mafundisho tanzu yenye kina na hivyo huu ukawa ni mwendelezo wa mkate wa uzima wa milele unaoendelea kumegwa kwa ajili ya wengi katika uhalisia wa maisha. Uinjilishaji Mpya unalitaka Kanisa kuonesha mwelekeo mpya katika kuishi na kimwilisha maisha na utume wake, kama anavyofanya kwa sasa Baba Mtakatifu Francisko!.









All the contents on this site are copyrighted ©.