2013-06-29 11:12:41

IMBISA na mchakato wa uchaguzi mkuu nchini Zimbabwe


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, IMBISA, hivi karibuni lilimtembelea na hatimaye, kuzungumza na Rais Josè Eduardo Dos Santos wa Angola kuhusu hali ya kisiasa Kusini mwa Afrika na kwa namna ya pekee, mchakato wa uchaguzi mkuu nchini Zimbabwe.

Hizi ni juhudi za IMBISA kukutana na kuzungumza na viongozi wakuu wa Serikali Kusini mwa Afrika, kama sehemu ya mbinu mkakati unaopania maboresho ya utawala bora, demokrasia, haki, amani na upatanisho wa kweli, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wanaoishi Kusini mwa Afrika. Itakumbukwa kwamba, wajumbe wa IMBISA wamekwisha kutana na kuzungumza na Rais Armando Guebuza wa Msumbiji. Ujumbe wa IMBISA ulikuwa chini ya uongozi wa Askofu Antonio Jaca Caxito wa Angola.

IMBISA inawataka viongozi wa SADC kuhakikisha kwamba, wanafanikisha uchaguzi mkuu nchini Zimbabwe na kwamba, uchaguzi huu unakuwa ni huru na wa haki. Malumbano ya viongozi wakuu wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa si dalili njema kwa ustawi na maendeleo ya wananchi wa Zimbabwe na Afrika katika ujumla wake.

Ujumbe wa IMBISA pia umeonesha wasi wasi kutokana na kinzani zinazoanza kufuka moshi kati ya Serikali na Chama cha Upinzani cha RENAMO, wanaotaka kurudi tena msituni kuendesha mapambano ya silaha nchini Msumbiji.







All the contents on this site are copyrighted ©.