Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya kumi na tatu ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa
Karibuni mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu tunapotafakari pamoja Liturujia ya Neno
la Mungu, Dominika ya 13 ya Mwaka C. Bwana wetu Yesu Kristo katika Injili anatangaza
upendo mkamilifu na utume wake wa kuwakoa watu kinyume na fikira za kibinadamu.
Mwanadamu
hufikiria mara moja kunakokuwa na kinzani, kuangamiza na hasa akiwa na nguvu zaidi
ya mpinzani wake. Kristu anapingwa na kunyanyaswa katika nchi iliyo yake na wanafunzi
wake wanapendekeza maangamizi dhidi ya wapinzani. Akitambua udhaifu wao anasema Mwana
wa Adamu hakuja kuangamiza roho za watu bali kuwaokoa watu na kuwapeleka mbinguni.
Akiendelea
katika utume wake anakutana na matukio mbalimbali na anatoa majibu ya kimungu. Tunamwona
mtu mmoja akifikiri kumfuasa Bwana ni raha msitarehe anamwomba Bwana akae katika msafara,
Bwana akijua hila yake anasema kama wataka kunifuata yakupasa kuwa tayari kulala hata
nje katika baridi na maana yake kuwa tayari kutoa maisha yako kwa sababu ya Injili.
Wanaposonga mbele anakutana na mtu mwingine anamwambia nifuate, mtu huyo anaweka
kikwazo cha kwanza kumzika Baba yake. Bwana anasema waache wafu wazike wafu wao. Katika
hili anataka mmoja ajitoe kikamilifu katika kuhudumu Injili yake si kuanza kubabaika
katika maisha mengine yasiyoambatana na Injili ya Bwana. Vivyo hivyo anakutana na
mtu mwingine anayeweka kikwazo cha kuwaaga wazazi na ndugu zake. Bwana anasema yakupasa
kuangalia mbele daima. Neema ya Mungu yatosha kwa ajili ya ndugu zako.
Mfululizo
wa watu mbalimbali wenye vikwazo mbalimbali wanaokutana na Bwana ni kielelezo cha
maisha ya wito katika Kanisa. Mara kadhaa watu mbalimbali huweka vikwazo kwa sauti
ya Mungu na hasa kwa sababu ya sauti nyingine zuizi. Kumbe ni vema kuzama katika tafakari
ili kupambanua sauti ya Mungu na kuitika mpango wa Mungu kadiri ulivyopangiwa. Jambo
la pili wito si lelemama, ni jambo la kukaza uso gumegume ukielekea Yerusalemu, ni
kushika njia ya msalaba, ni utumishi na si kutumikiwa. Ni kufuatilia mpango wa kichungaji
wa Bwana wetu Yesu Kristo.
Mpendwa mwanatafakari ndiyo kusema mpango wa kichungaji
wa Bwana ni kuokoa watu walio katika taabu ili waungane na walio katika neema. Ni
kuendeleza mpango wa Mungu tangu uumbaji aliposema kila kitu ni chema. Kumbe, kuangamiza
watu au viumbe vingine ni kwenda kinyume na mpango wa Mungu. Kristo ni mkombozi na
si mwangamizi, Kristo ni mwalimu na mzazi apendaye maisha ya watoto wake yashamiri
na kusonga mbele mpaka mwisho wa dahari. Kristo anapoita ili kumfuata ni lazima kuondokana
na uzembe na ulegevu usio na msingi wa imani.
Mara kadhaa inajitokeza baadhi
ya washika ofisi za Kanisa kuwa wavivu na watu wanaodeka, katika Injili ya leo Bwana
anakemea jambo hilo akisema mbweha wana mahali pakuweka vichwa vyao lakini Mwana wa
Adamu hana! Ni lazima mpendwa msikilizaji kujikana na kujikatalia katika maisha ya
kumfuasa Bwana.
Mtakatifu Paulo akitafakari Neno la Bwana anawaambia Wagalatia
kuwa Bwana ametuweka huru na hivi kwa nini tunaswe tena chini ya kongwa la utumwa?
Yatupasa kuondokana na vikwazo hivyo vinavyo komaza mwendelezo wa ulaghai na uvivu
wa kumtumikia Mungu. Katika somo la kwanza tunapata habari ya Elisha anaitwa na Mungu
na mara anaacha mali yake na kuanza safari ya utumishi kwa ajili ya wokovu wa watu.
Kwa namna ya Elisha nasi twapaswa kuchangamkia wito wetu tulioupokea wakati wa Ubatizo.
Mpendwa Ubatizo si lelemama bali ni wajibu msingi na wa kwanza katika maisha yako.
Unapaswa kuupalilia daima ili kwao ukafike mbinguni.
Nikutakie yote mema ukichuchumalia
baraka za Mungu na neema zake kwa ajili ya kutengeneza wito wako. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari
hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.