2013-06-28 09:19:08

Pallio Takatifu ni alama ya Kristo mchungaji mwema, anayemtafuta Kondoo aliyepotea ili aweze kumbeba mabegani mwake!


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Sherehe ya Watakatifu Petro na Paulo miamba wa Imani, Jumamosi asubuhi, tarehe 29 Juni 2013, anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican pamoja na kutoa Pallio Takatifu kwa Maaskofu wakuu, 34 na kati yao kuna 3 kutoka Barani Afrika. Askofu mkuu Francois Xavier Le Van Hong kutoka Vietnam atapelekewa Pallio Takatifu Jimboni mwake.

Ibada ya kuwavika Maaskofu wakuu Pallio Takatifu ni ile iliyofanyiwa marekebisho na kuidhinishwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kunako mwaka 2012. Ibada hii imefupishwa ili kutoa nafasi kwa waamini kuweza kushiriki kikamilifu katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu bila kukatishwa katishwa!

Ibada ya kuwavika Maaskofu wakuu Pallio Takatifu, itaanza kwa kusomwa orodha ya majina ya Maaskofu wakuu wapya na baadaya hapo utafuatia wimbo wa kuingilia na baadaye, Kardinali atawatambulisha Maaskofu wakuu kwa Baba Mtakatifu, ili awapatie Pallio takatifu kielelezo cha ukuu wa Majimbo Makuu wanaoyaongoza na Utii na Umoja na Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Maaskofu wakuu wapya watakula kiapo cha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Pallio Takatifu zitabarikiwa na baadaye Maaskofu wakuu watavishwa na Ibada ya Misa Itaendelea kwa wimbo wa Bwana utuhurumie. Ikumbukwe kwamba, hii si Ibada ya Kisakramenti ambayo kimsingi inafanywa mara baada ya mahubiri, kama inavyojionesha wakati wa kupokea Sakramenti ya Ubatizo, Kipaimara, Ekaristi Takatifu au Upadrisho.

Kimsingi Pallio Takatifu ni kitambaa cha sufu safi kinachoshonwa kwa mikono. Mwanzoni ilimaanisha kuwa ni Kondoo aliyepotea; ni alama pia ya Kristo mchungaji mwema. Ni alama iliyoanza kutumika kunako Karne ya nne, nyakati za uongozi wa Papa Gregori wa Saba, wakati ambapo Maaskofu wakuu walikuwa wanafika mjini Roma kwa ajili ya kupokea Pallio Takatifu.

Papa Paulo wa sita, akafanya marekebisho makubwa, Pallio takatifu ikaanza kutolewa kwa Maaskofu wakuu wa Majimbo makuu tu!







All the contents on this site are copyrighted ©.