2013-06-28 14:44:04

Changieni ustawi na maendeleo ya majimbo yenu!


Askofu Joseph Mbatia wa Jimbo Katoliki la Nyahururu, Kenya, amewataka waamini wanaoishi nje ya Majimbo yao kuhakikisha kwamba, wanasaidia kuchangia mchakato wa ustawi na maendeleo ya Majimbo yao na kamwe wasisahau walikotoka. Hii ni changamoto ya kuendelea kuchangia kwa hali na mali maendeleo ya maeneo walikotoka.

Askofu Mbatia ameyasema hayo hivi karibuni wakati alipokuwa anaadhimisha Ibada ya Misa takatifu kwa ajili ya waamini wanaotoka Jimbo Katoliki la Nyahururu, nchini Kenya kwenye Kikanisa cha Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Mtakatifu Paulo, Kilichoko mjini Nairobi.

Askofu Mbatia alitumia fursa hii kufafanua baadhi ya miradi iliyoibuliwa na Jimbo Katoliki Nyahururu kama sehemu ya mchakato wa kutaka kujitegemea na kulitegemeza Kanisa katika maisha na utume wake, hasa wakati huu, wanapoendelea kusonga mbele kwa imani na matumaini ya kusimama kwa miguu yao wenyewe ili kupunguza ufadhili kutoka nje ya nchi.

Jimbo limebuni mradi utakaogharimu kiasi cha shilingi million 140 hadi utakapokamilika; mradi ambao kila mwanajimbo anaalikwa kuchangia ndiyo maana anawaalika waamini kutoka Jimboni humo kushirikishi kikamilifu katika kuchangia kwa hali na mali.

Askofu Mbatia anawaalika waamini kujiwekea akiba mbinguni kwa njia ya sadaka na matendo ya huruma kwa jirani na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Anawakumbusha kwamba, hapa duniani, kila mtu ni mpita njia!








All the contents on this site are copyrighted ©.