2013-06-27 09:55:40

Rais Barack Obama kutembelea Afrika ya Kusini?


Wakati wananchi wa Afrika ya Kusini na wapenda amani kutoka sehemu mbali mbali duniani wanapoendelea kuyaelekeza masikio yao nchini Afrika ya Kusini kutokana na hali ya Mzee Madiba kuendelea kudhohofu zaidi, Rais Barack Obama wa Marekani, katika safarai yake ya kikazi Barani Afrika, anatarajiwa kutembelea Afrika ya Kusini mwishoni mwa Juma.

Ratiba inaonesha kwamba, Rais Obama atatembelea Johannesburg na Cape Town, Jumamosi na Jumapili. Serikali ya Afrika ya Kusini hajazungumzia kuhusu mabadiliko ya ratiba hii kutokana na kudhohofu kwa Rais Mstaafu Nelson Mandela. Wananchi wa Afrika ya Kusini wanasema, kwa sasa wanamwachia Mwenyezi Mungu maisha ya Mzee Madiba atende kadiri ya mapenzi yake.

Hata ikiwa kama atafariki, lakini wananchi wa Afrika ya Kusini wanapaswa kusherehekea zawadi ya maisha ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia Mzee Madiba ambaye ameonja, magumu na raha za dunia. Miaka 27 ya taabu na mateso kizuizini si haba! Miaka 5 ya uongozi kama Rais, ni neema na baraka!

Rais Obama amewasili mjini Dakar, Senegal tarehe 26 Juni 2013 na atakuwemo nchini humo hadi tarehe 28 Juni 2013 atakapoanza safari yake kuelekea Afrika ya Kusini na Tanzania, wakati huu anapofanya ziara rasmi kwa ajili ya kutembelea Bara la Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.