2013-06-27 07:33:48

Mshikamano wa upendo na maskini kutoka sehemu mbali mbali za dunia!


Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani linawaalika waamini kuunga mkono jitihada za Baba Mtakatifu Francisko za kutaka kuonesha mshikamano wa upendo na maskini pamoja na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kwa njia ya sadaka na majitoleo yao. RealAudioMP3

Itakubukwa kwamba, Maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu Petro na Paulo miamba wa imani hapo tarehe 29 Juni kila mwaka, waamini wanaalikwa kuonesha mshikamano na Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa kutoa mchango, unaomwezesha Baba Mtakatifu kuonesha mshikamano wa upendo na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Baba Mtakatifu Francisko anapenda kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini wa hali na kipato katika maisha na utume wake, changamoto kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kumuunga mkono. Nchini Marekani, waamini watakusanya mchango wao kuanzia Jumamosi tarehe 29 hadi 30 Juni 2013, kwa kuongozwa na kauli mbiu “Iweni mahujaji wa upendo”.

Kwa njia hii, waamini wataweza kushiriki katika mchakato unaopania kuwashirikisha wengine upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Sadaka ya siku hii inawawezesha waamini kuonja shida na mahangaiko ya jirani zao kutoka sehemu mbali mbali za dunia anasema Askofu mkuu Dennis Schnurr, Mwenyekiti wa michango, Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani.

Anakumbusha kwamba, haba nah aba hujaza kibaba! Kila mwamini akichangia kwa moyo wa ukarimu na upendo, mchango unakuwa mkubwa kiasi ambacho Kanisa linaweza kugharimia mikakati ya maendeleo na shughuli za kichungaji kwa: waathirika wa vita, majanga asilia, madhulumu ya kidini pamoja na kuendelea kugharimia majiundo ya Makleri, Watawa na Makatekista, wadau wakuu wa Uinjilishaji Mpya.

Baba Mtakatifu Francis katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Pasaka kwa Mwaka 2013 aliwaalika waamini kuwa kweli ni mawakala wa huruma ya Mungu kwa kuwa ni vyombo ambavyo vitaweza kutumiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili kulowanisha dunia, kulinda na kutunza mazingira; kudumisha na kuendeleza misingi ya haki, amani na upatanisho wa kweli.








All the contents on this site are copyrighted ©.