2013-06-27 07:42:33

Mafundisho Jamii ya Kanisa na utandawazi!


Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, hivi karibuni alihudhuria mkutano uliokuwa umeandaliwa na Taasisi ya Lumen Christi ya Chuo Kikuu cha Chicago, Marekani ili kujadili pamoja na mambo mengine athari za utandawazi katika nchi zinazoendelea, njia madhubuti zinazopaswa kuchukuliwa na Jumuiya ya Kimataifa katika kujenga uchumi unaokubalika kimaadili.

Kardinali Turkson anabainisha kwamba, Kanisa lina dhamana na wajibu wa kuwakumbusha viongozi wa kimataifa kwamba, maskini duniani wanapaswa kuheshimiwa, kuthaminiwa na kusaidiwa ili kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali za maisha kwa njia ya mshikamano unaoongozwa na kanuni ya auni; utu wa mtu na maadili vikipewa kipaumbele cha kwanza.

Mama Kanisa anapozungumza masuala mbali mbali yanayomgusa mwanadamu, kwa kawaifa anawaelekea watu wote wenye mapenzi mema, kama ilivyokuwa katika Mafundisho ya Waraka wa Papa Yohane wa Ishirini na tatu, Pacem in Terris, Amani Duniani.

Kardinali Turkson anasema, Mafundisho Jamii ya Kanisa ni amana na utajiri mkubwa unaopata chimbuko lake katika miaka 1891 kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa: maisha, utu na heshima ya binadamu. Ni mafundisho yanayobubujika kutoka katika majadiliano kati ya imani na akili ya mwanadamu, ili kumuenzi mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Mafundisho haya yanajikita kwa namna ya pekee katika haki, amani, upendo na upatanisho.

Ni mafundisho ambayo yanajenga msingi wake kutoka katika Maandiko Matakatifu na Maadili. Yanaonesha haki na wajibu; mafao ya wengi na kwamba, sera za maendeleo endelevu zinapaswa kumgusa mtu mzima: kiroho na kimwili kwani tatizo kubwa katika ulimwengu wa utandawazi ni ukosefu wa usawa kati ya watu hali inayopelekea kinzani na migogoro ya kijamii.

Usawa ni kikolezo kikubwa cha msingi wa maendeleo, lakini kwa miaka mingi wachumi wengi wameliangalia jambo hili kwa jicho la makengeza. Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kubainisha kwamba, utu na heshima ya binadamu vinapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika mipango ya maendeleo endelevu.

Kardinali Turkson anaendelea kubainisha kwamba, Jamii nyingi zinakabiliana na changamoto za utandawazi katika medani mbali mbali za maisha, changamoto inayojionesha kwa kasi ya ajabu katika masuala: uharibifu wa mazingira; ongezeko kubwa na wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum wanaotafuta maboresho na hifadhi ya maisha; kuna mwingiliano mkubwa katika njia za mawasiliano ya jamii, kiasi kwamba, leo hii dunia imekuwa kama Kijiji, bila kusahau kwamba, kuna kiasi kikubwa cha fedha na mtaji kinachovuka mipaka ya nchi kama: mtaji, habari, kazi, mali ghafi na bidhaa.

Utandawazi unaopaswa kuungwa mkono ni ule unaoshirikisha utajiri wa watu na tamaduni zao kuendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya ulimwengu mamboleo; huku uhuru, utu na heshima ya mwanadamu vikipewa msukumo wa pekee. Binadamu kamwe anasema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kuwa ni mdau wa utandawazi na wala si mwathirika wa utandawazi, anayetenda kwa kuongozwa na mwanga wa akili timamu, upendo na ukweli. Mafao ya wengi na upendeleo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ni jambo la kuzingatiwa kwa kumwilisha mshikamano unaoongozwa na kanuni ya auni.

Kardinali Turkson anaendelea kubainisha kwamba, utandawazi umekuwa ni chanzo cha kukua na kuenea kwa umaskini, kinzani na migawanyiko. Hii inatokana na ukweli kwamba, hakuna mgwanyo sawa wa rasilimali ya dunia. Kwa mfano utajiri na rasilimali inayopatikana Barani Afrika na kutoka katika nchi zinazoendelea zimezitajirisha kwa kiasi kikubwa Nchi Tajiri duniani na Afrika ikaendelea kutumbukia katika umaskini, magonjwa na njaa.

Ni Bara ambalo liliathirika kwa kiasi kikubwa na biashara haramu ya utumwa, leo hii kuna utumwa mamboleo. Ili utandawazi uweze kuwanufaisha watu wengi zaidi duniani, kuna haja ya kuhakikisha kwamba, hata nchi changa zaidi duniani zinashiriki katika mchakato wa maoni, maamuzi na utekelezaji wa mikakati inayowagusa. Huu ndio utandawazi unaowajibisha.

Utandawazi umekuwa ni chanzo cha imani kwa wananchi wengi wanaoishi katika nchi changa duniani. Leo wengi wao ni waamini wa dini na madhehebu mbali mbali hata kama kuna baadhi ya watu wameendelea kubaki katika dini na imani zao za asili. Utandawazi umesaidia pia mwingiliano wa shughuli za uchumi, biashara na masoko. Lakini, nchi hizi zinaendelea kunyonywa na kuwafaidisha wachache ndani ya Jamii, ambayo wamejikuta wakiogelea katika kashfa za rushwa na ufisadi wa mali ya umma. Makampuni makubwa ya kimataifa yamekuwa ni wakwepaji wakubwa wa kodi ambayo ingeweza kusaidia mchakato wa maendeleo endelevu kwa nchi changa duniani.

Kutokana na ukweli huu, anasema Kardinali Turkson kuna haja ya kuzingatia kanuni maadili katika masuala ya utandawazi kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Mungu na mwanadamu; kwa kuibua sera za uchumi zinazozingatia haki, utu na heshima ya mwanadamu; kazi ipewe heshima yake na wafanyakazi wapate ujira unaokidhi mahitaji muhimu ya mwanadamu.

Mali itumike kwa ajili ya mafao ya wengi, kwa kuzingatia mshikamano unaosimamiwa na kanuni ya auni, upendo na udugu bila kusahau kwamba, kuna haja ya kujipatanisha na Mungu na jirani, ili kujenga na kuimarisha msingi wa utawala bora unaozingatia sheria na kanuni za nchi.

Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani anasema, athari za utandawazi mintarafu Mafundisho Jamii ya Kanisa zinaweza kuangaliwa katika misingi ya haki, mali, mshikamano, udugu, upatanisho, utawala bora na kanuni ya auni. Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican iwe ni fursa ya kujichotea utajiri unaofumbatwa katika Nyaraka mbali mbali za Mtaguso huo kwa maisha na utume wa Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko anawahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema: kwanza kabisa kuwapenda na kuwathamini maskini; kusimama kidete kulinda na kutetea amani sanjari na utunzaji bora wa mazingira. Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kushirikiana kwa dhati mintarafu mpango wa Mungu, aliyeumba na kuona kwamba, kila kitu alichokuwa ameumba ni chema na kizuri.

Makala hii imeandaliwa na
Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.