2013-06-27 12:21:31

Jitahidini kumfahamu Kristo ambaye ni mwamba amini, chemchemi ya furaha na uhuru wa kweli!


Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Ibada ya Misa takatifu, Alhamisi tarehe 27 Juni 2013 kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican amewakumbusha waamini kukita imani yao katika mwamba thabiti ambao ni Yesu Kristo na kwamba, hakuna Ukristo pasi na Kristo! Ni mwaliko kwa waamini kuonesha ile furaha ya maisha yao kwa Kristo na Kanisa lake, kwani Kristo hapendi kuwaona watu "wenye nyuso zilizokunjamana kama kigae na mioyo migumu kama jiwe"!

Wakristo wanapaswa kutolea ushuhuda wa imani yao kwa njia ya matendo na kujipambanua kwa kusimama kidete kulinda na kutetea ukweli. Wakristo wanaoonesha imani yao kwa njia ya matendo thabiti ni sawa na mjenzi aliyejenga nyumba yake kwenye mwamba thabiti, kamwe haitaweza kutikisika. Mwamba huu ni Neno la Mungu. Lakini, wale wanaopepeta mdomo katika maisha yao, watambue kwamba, wanajenga nyumba katika mchanga na anguko lao ni kubwa!

Baba Mtakatifu anasema kwamba, wale wanaomtegemea Kristo mwamba na ngome ya maisha yao, wataweza kuvuka magumu ya maisha, hawa ndio Wakristo ambao wanamkumbatia na kumwamini Kristo na kamwe hawezi kuwadanganya. Kuna Wakristo wanaojiita kuwa ni Wakristo lakini hawamwamini Kristo, hawa ni wale wanaopotoka na kielelezo cha utepetevu wa imani katika ulimwengu mamboleo. Kwa bahati mbaya anasema Baba Mtakatifu waamini kama hawa wamo hata ndani ya Kanisa.

Baba Mtakatifu katika mahubiri yake amekazia kwa na namna ya pekee: umuhimu wa kumfahamu Yesu Kristo ambaye ni mwamba amini, chemchemi ya uhuru wa kweli na watu wenye furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo, furaha ambayo wanawashirikisha wengine.

Ibada hii ya Misa takatifu imehudhuriwa na viongozi na wafanyakazi kutoka katika idara ya afya mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.