2013-06-26 11:17:41

Makleri wanachangamotishwa kuwa ni mababa wa neema na maisha ya kiroho katika utekelezaji wa shughuli za kichungaji!


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, kilichoko mjini Vatican, siku ya Jumatano asubuhi, tarehe 26 Juni 2013, amewachangamotisha waamini kuhakikisha kwamba, wanakuza ndani mwao ile furaha ya kujisikia kwamba ni wazazi, jambo ambalo pia linapaswa kujionesha hata katika maisha ya Makleri ambao kimsingi wanapaswa kuishi maisha ya useja. Kama hakuna furaha ya kuwa baba, anasema Papa Francisko, hapo kuna kitu ambacho hakiendi sasa sawa!

Baba Mtakatifu anasema, ubaba wa Makleri unajionesha katika utekelezaji wa mikakati na majukumu ya shughuli za kichungaji. Hawa ni mababa wa maisha ya kiroho wanaoshiriki dhamana ya kuwa ni mababa. Mababa wa familia wanalo jukumu la kuhakikisha kwamba, wanalea, wanatunza na kuzihudumia familia zao, changamoto kwa waamini kuomba neema ya kuwa kweli ni mababa wema na waaminifu wa familia.

Baba Mtakatifu anakiri kwamba, kuna dhambi na mapungufu mengi yanayofanywa na mababa, lakini jambo moja kubwa ni kwamba, wanaunganishwa na ile hamu ya kuwa ni mababa hata kama hawana watoto wao wa kuzaa! Makleri wawe ni mababa wa neema na maisha ya kiroho katika shughuli za kichungaji ndani ya Kanisa.

Kama Makleri, wanayo haki ya kumshukuru Mwenyezi Mungu anayewakirimia zawadi ya kuwa ni mababa wa maisha ya kiroho ndani ya Kanisa. Abraham, Baba wa imani ni kielelezo makini cha baba mwenye dhamana ya kulinda na kutetea familia. Mzee Simeoni anaonesha ile liturujia ya furaha kwa kumwimbia Mwenyezi Mungu pale anapompokea Mtoto Yesu alipopelekwa Hekaluni.







All the contents on this site are copyrighted ©.