2013-06-26 09:07:25

Hakuna kulala hadi Kanisa liweze kujitegemea!


Kardinali John Njue, Askofu mkuu wa Jimbo Kuu la Nairobi anaendelea kuwahimiza waamini nchini Kenya na Afrika kwa ujumla kuhakikisha kwamba, wanajifunga kibwebwe kulitegemeza Kanisa katika maisha na utume wake wa Uinjilishaji wa kina, unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kwa miaka mingi Wamissionari wamejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kupandikiza mbegu ya imani ya Kikristo, wakaikuza na kuipalilia sasa ni dhamana na jukumu la Waamini Barani Afrika kujitegemea na kulitegemeza Kanisa.

Kardinali Njue ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa anatabaruku Kanisa la Parokia ya Mtakatifu Yosefu Mkasa, lililoko eneo la Kahawa Magharibi, Jijini Nairobi. Amewashukuru na kuwapongeza waamini wa Parokia hii kwa kuonesha moyo wa ukarimu uliowawezesha kujenga Kanisa kwa nguvu zao wenyewe bila ya kuhitaji msaada kutoka nje ya nchi. Parokia hii itahudumiwa na Wamissionari wa Consolata.

Waamini wa Parokia ya Mukasa wanaendelea kuhamasishwa kuhakikisha kwamba, wanakua na kuimarisha ari na wito wa shughuli za Kimissionari, kwani hapa hakuna kulala hadi kieleweke! Watu wanasubiri kusikia Habari Njema ya wokovu inatangazwa kwa ari kubwa zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao, kama kielelezo cha imani tendaji, hasa wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.