2013-06-26 07:35:13

Damu ya Azizi ya Kristo ni chemchemi ya Upatanisho


Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika Waraka wake Africae Munus, Dhamana ya Afrika anasema kwamba, haki, amani na upatanisho ni mawazo makuu yaliyochaguliwa na Mababa wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika kwa kutambua wajibu na dhamana ya Kanisa Barani Afrika katika wajibu wake wa kijamii na kitaalimungu. RealAudioMP3
Upatanisho na haki ni misingi mikuu ya ujenzi wa amani. Amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayowajibisha binadamu. Amani bila haki ni kudanganyana na wala haiwezi kudumu kwa muda mrefu. Haki ya binadamu inapaswa kuwa ni tunda la upatanisho katika ukweli unaoongozwa na upendo. Haki ni fadhila fungamanishi katika maisha ya binadamu.
Bila nguvu ya upatanisho anaendelea kusema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kwamba, mikakati na mchakato wa amani unakosa nguvu, mwelekeo na dira. Toba na wongofu wa ndani ni jambo la msingi linaloweza kujenga na kuimarisha misingi ya haki na amani, kwa kutambua nafasi na uwepo wa Mungu katika hija hii ya maisha ya mwanadamu.
Upatanisho unapata chimbuko lake katika upendo wa dhati, kama inavyojionesha katika maisha na utume wa Yesu ambaye ni Mpatanishi kati ya Mungu na binadamu. Upatanisho unamwezesha mwanadamu kujenga umoja na mshikamano wa kweli, changamoto kwa waamini kuwa kwelini wajumbe wa upatanisho.
Bara la Afrika kwa miaka mingi limejikuta likitumbukia au kutumbukizwa katika kinzani, migogoro, vita na mafarakano, mambo ambayo yameacha madonda ya kudumu katika maisha na mioyo ya watu, kumbe, upatanisho unapaswa kuwa ni mchakato endelevu katika maisha na utume wa Kanisa Barani Afrika. Upatanisho hushinda matatizo, hurudisha heshima ya watu binafsi na hufungua njia ya maendeleo na amani ya kudumu kati ya watu katika ngazi mbali mbali. Upatanisho linapaswa kuwa ni tendo la kijasiri. Wahanga wana haki ya kujua ukweli na kupata haki.
Ni katika mantiki hii, Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania, kuanzia tarehe 26 hadi tarehe 29 Juni 2013, kwenye Chuo Cha Mtakatifu Gaspar, Kola, Morogoro, litakuwa na Semina kuhusu Damu ya Kristo chemchemi ya Upatanisho. Lengo ni kuendeleza tafakari ya kina iliyotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, itakayowawezesha waamini kuwa na maisha mapya katika Kristo, ambaye ndiye Mpatanishi mkuu kati ya Mungu na binadamu. Damu ya Kristo ni mto wa rehema.
Haya pia ni maandalizi ya Maadhimisho ya Mwezi Julai, ambao kimsingi umetengwa na Mama Kanisa kwa ajili ya Ibada kwa Damu Azizi ya Kristo; mwezi ambao unafunguliwa kwa Siku kuu ya Damu Azizi ya Yesu inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe Mosi, Julai. Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu linajiandaa kuadhimisha Jubilee ya miaka 200 tangu lilipoanzishwa, yaani tangu Mwaka 1815 hadi mwaka 2015. Upatanisho uwe ni mwanzo mpya katika Kristo Mpatanishi.








All the contents on this site are copyrighted ©.