2013-06-25 08:27:30

Ulinzi na usalama kwa mahujaji ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani!


Kamati ya Maandalizi kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa mwaka 2013 huko Rio de Janeiro, Brazil, yanayotarajiwa kuanza kushika kasi hapo tarehe 22 hadi tarehe 28 Julai 2013 inasema, ulinzi na usalama wa mahujaji na wananchi katika ujumla wao, unapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza na vikosi vya ulinzi na usalama, ili kuhakikisha kwamba, tukio hili la kihistoria linaadhimishwa katika mazingira ya: Ibada, amani na utulivu.

Serikali ya Brazil imesema kwamba, vikosi vya ulinzi na usalama vimekwisha jiandaa kwa ajili ya maadhimisho haya na kwamba, askari wamekwisha kupangiwa maeneo ya ulinzi na usalama katika maeneo ambayo yatatumika kwa ajili ya: Ibada, Katekesi na malazi. Wizara ya Mambo ya ndani ya nchi kwa kushirikiana na Wizara ya Ulinzi na Usalama wamepewa dhamana ya kuhakikisha kwamba, ulinzi na usalama vinadumishwa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani inayoongozwa na kauli mbiu " Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa ni wanafunzi".

Dr. Domenico Giani, Kamanda wa Vikosi vya Ulinzi na usalama vya Vatican anasema kwamba, wanaendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na Serikali ya Brazil ili kuhakikisha kwamba, Maadhimisho haya yanakwenda kama yalivyopangwa. Katika siku za hivi karibuni wananchi wa Brazil wamekuwa wakifanya maandamano kupinga ongezeko la gharama ya maisha kutokana na maandalizi ya Kombe la Dunia litakalofanyika nchini humo kunako mwaka 2014, kwamba, hayana uhusiano wowote na Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani.

Hili ni tukio la Kiimani linalosubiriwa na wananchi wengi wa Brazil, anasema Askofu mkuu Joao Oran Tempesta, wa Jimbo kuu la Rio de Janeiro, ambaye pia ni Rais wa Kamati ya Maandalizi kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil. Vijana wanaoandamana nchini Brazil wanataka kujenga utamaduni utakaowaletea matumaini ya leo na kesho iliyo bora zaidi; wanataka umoja, upendo na mshikamano wa kweli. Kwa vijana Wakatoliki, Kristo anapaswa kuwa ni lengo lao kuu katika hija ya maisha yao!

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani yanawashirikisha vijana wenye fadhila za Kikristo, wanaotamani kuleta mabadiliko duniani kwa kuzingatia kwanza kabisa: haki na amani; utu na heshima ya binadamu pamoja na mafao ya wengi. Askofu mkuu Joao Oran Tempesta anasema, maandamano haya ni dalili kwamba, wananchi hawaridhiki na jinsi ambavyo Serikali inavyoshughulikia masuala ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Wanasikitishwa na kuenea kwa rushwa na ufisadi. Serikali ya Brazil inaendelea kufanya majadiliano na waandamanaji hao ili kupata suluhu ya kudumu.







All the contents on this site are copyrighted ©.