2013-06-25 07:47:08

SIGNIS yafuta Kongamano la Kimataifa huko Beirut kutokana na vita inayoendelea Syria


Kongamano la Kimataifa lililokuwa limeandaliwa na Shirikisho la Wanahabari Wakatoliki Kimataifa, SIGNIS, ambalo lilitarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 20 hadi tarehe 23 Oktoba 2013 mjini Beirut, nchini Lebanon, limefutwa kutokana na machafuko ya kivita yanayoendelea kupamba moto huko Syria.

Waandaaji wa kongamano hili pia nchini Lebanon walionesha hali ya wasi wasi wa usalama wa wajumbe wa SIGNIS kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Mambo haya yote yamepelekea kufutwa kwa Kongamano hili, kama alivyoeleza Bwana Augustine Loorthusamy, Rais wa SIGNIS.

Wamesikitishwa na uamuzi huu, lakini SIGNIS inapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati na wananchi wa Syria wanaokabiliana na hali ngumu ya maisha kutokana na vita inayoendelea huko Mashariki ya Kati. Wanasema, wanaendelea kuwasindikiza kwa njia ya sala na kwamba, Wakristo huko Mashariki ya Kati wanao wajibu na dhamana ya kubaki na kuendeleza nchi yao, ingawa maeneo mengi yameharibiwa kutokana na vita.

Huu ni mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inaendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini, upatanisho, haki na amani; wananchi wanapaswa kuhamasishwa kutumia njia mbadala badala ya kukimbilia mtutu wa bunduki kama suluhu ya kinzani na migogoro inayojitokeza huko Mashariki ya Kati. Wananchi wamechoka na vita wanataka kuonja amani na matumaini mapya.

Licha ya Kongamano hili la Kimataifa kufutwa, bado wajumbe wa SIGNIS watakutana katika mji utakaopangwa baadaye. Hadi sasa Roma na Madrid ni kati ya miji inayopewa kipaumbele cha kwanza.







All the contents on this site are copyrighted ©.