2013-06-25 15:09:40

Papa Francisko asema: Ukristo ni wito wa upendo!


Ukristo ni wito unaoonesha upendo wa Mungu kwa binadamu na kwamba, Yesu daima atawasaidia wale wanaomkimbilia kwa imani na matumaini; hata katika shida na magumu, hakuna haja ya kukata tamaa, bali kupiga moyo konde na kusonga mbele kwa ujasiri mkuu.

Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, Jumanne, tarehe 25 Juni 2013, kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican.

Baba Mtakatifu akifanya rejea kwenye Liturujia ya Neno la Mungu anawaomba waamini na watu wenye mapenzi mema kuwa na busara kama iliyooneshwa na Babu Abraham kwa kukumbatia amani pamoja na kujisalimisha mikononi mwa Mwenyezi Mungu. Abraham ni kielelezo cha imani, matumaini na mapendo, hali ambayo ilimwezesha kuwa ni Baba wa Mataifa.

Mwenyezi Mungu anaongea na kila mwamini mmoja mmoja, kwani ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Kila Mkristo ameitwa binafsi na hakuna cha bahati mbaya, bali kila kitu ni sehemu ya mpango wa Mungu; ni wito unao andamana na ahadi pamoja na wajibu! Baba Mtakatifu anasema, Yesu Kristo ni kielelezo makini cha wito na wajibu huu kwani hata katika maisha yake alikumbana na vikwazo na kinzani lakini hakukata tamaa kwani alimtegemea Mwenyezi Mungu katika kutekeleza kazi ya ukombozi.

Waamini wanapaswa kujiaminisha kwa Mwenyezi Mungu ambaye ni uhakika wa usalama wa maisha yao. Ukristo ni witona mwaliko wa upendo unaomwezesha mwamini kuwa ni Mtoto mpendwa wa Mungu; ndugu yake Kristo. Ni wito ambao una raha, magumu na changamoto zake. Jambo la msingi ni kila mwamini kuhakikisha kwamba, anakuwa mwaminifu kwa Kristo na Kanisa lake, kama alivyokuwa Abraham, Baba wa imani.

Waamini wajitahidi kutunza ahadi za Ubatizo katika maisha yao. Pale wanapotumbukia katika dhambi, wawe na ujasiri wa kusimama na kumwendea Yesu kwa moyo wa toba na majuto, kwani amewaahidia wafuasi wake kwamba, atakuwa pamoja nao hadi utimilifu wa nyakati.

Ibada ya Misa takatifu imehudhuriwa na viongozi waandamizi na wanafanyakazi kutoka Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum, Taasisis ya Kipapa kuhusu maisha pamoja na kituo cha unajimu cha Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.