2013-06-22 09:46:22

Vurugu na madhulumu ya kidini, si bure kuna mkono wa mtu kutoka Nje!


Kardinali John Onaiyekan, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria, hivi karibuni akishiriki katika mkutano wa majadiliano ya kidini kati ya Wakristo na Waislam uliokuwa umeandaliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Oasis, Jimbo kuu la Milano, alisema kwamba, kinzani, vurugu na mashambulizi yanayofanywa na baadhi ya waamini wa dini ya Kiislam wenye misimamo mikali ya kidini nchini Nigeria, Syria na kwingineko ni mambo ambayo yanapandikizwa kutoka nje.

Mfuko wa Kimataifa wa Oasis, hivi karibuni uliwakusanya viongozi wakuu wa dini ya Kiislam na Kikristo ili kujadili kwa pamoja mbinu mkakati unaoweza kufanyiwa kazi ili waamini wa dini hizi mbili waweze kuishi kwa amani, upendo na mshikamano kama ilivyokuwa hapo awali, ambapo watu waliheshimiana na kuthaminiana hata katika tofauti za dini na imani zao.

Lakini kwa miaka ya hivi karibuni mambo yamebadilika sana, kinzani, migogoro na mauaji kwa kisingizio cha imani yameshika kasi kubwa sehemu mbali mbali za dunia.

Wakristo na Waislam nchini Nigeria waliishi kwa amani na utulivu, hadi miaka ya hivi karibuni hali ya hewa ilipochafuka baada ya kuibuka kwa Kikundi cha Boko Haram ambacho tafsiri yake kwa lugha ya Kiswahili ingeweza kuwa ni "Elimu ya nchi za Magharibi ni dhambi". Hiki ni Kikundi kinachopania kuhakikisha kwamba, Nigeria inatawaliwa kwa "SHARIA" ya dini ya Kiislam. Kikundi hiki kilianzishwa kunako mwaka 2002.

Tangu mwaka 2009 hadi sasa kuna zaidi ya watu 2,800 ambao wamepoteza maisha yao kutokana na madhulumu ya kidini. Boko Haram mwanzoni hakikuwa ni kikundi cha kigaidi, lakini pole pole kilianza kukataa kushirikiana na waamini wa dini nyingine na hivyo kujitenga na matokeo yake, kikaanza kujiingiza katika madhulumu ya kidini. Hiki ni kikundi ambacho kinapata misaada ya hali na mali kutoka nje ya nchi.

Kuna baadhi ya raia kutoka nchi za nje wamekamatwa nchini Nigeria wakiwa wanamiliki ghala kubwa ya silaha za kivita, huko Kano. Huu ndio mwelekeo wa vikundi vya kigaidi kama Al Shabaab, kama kinavyojulikana Somalia; Al Qaeda, Mashariki ya Kati; Taliban huko Pakistan. Ni Kikundi cha hatari kwani kinafanya mauaji kwa wote bila kujali kitu.

Lakini ikumbukwe kwamba, si waamini wote wa dini ya Kiislam wanaunga mkono Kikundi cha Boko Haram, Al Shabaab au Al Qaeda, kwani hawa wanachafua dini na imani ya Kiislam kwa ajili ya masilahi yao binafsi, anasema Kardinali John Onaiyekan. Kuna haja kwa waamini wa dini mbali mbali kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; haki na amani pamoja na mafao ya wengi. Waamini washirikiane kwa dhati katika mambo msingi na tofauti zao isiwe ni kisingizio cha kuanzisha fujo na madhulumu bali utajiri unaopaswa kufanyiwa kazi kwa ajili ya mafao na ustawi wa Jamii nzima.








All the contents on this site are copyrighted ©.