2013-06-22 09:22:15

Kanisa halina budi kujitegemea ili kutekeleza mikakati ya Uinjilishaji wa kina!


Kardinali John Njue, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Nairobi anasema, umefika wakati kwa Kanisa nchini Kenya kujitegemea kama sehemu ya mchakato wa kuendeleza shughuli za Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Kardinali Njue ameyasema hayo hivi karibuni wakati alipokuwa anazindua Jengo la Kituo cha Pacis, lenye urefu wa ghorofa sita, litakalotumiwa na Kampuni ya Bima ya Pacis inayomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki Kenya.

Kardinali Njue anasema kwamba, Kampuni hii itakuwa ni kitega uchumi kikubwa kwa Kanisa Katoliki nchini Kenya, kitakachokuwa na uwezo wa kusaidia kutoa ajira kwa vijana pamoja na maboresho katika sekta ya elimu, afya, maendeleo na huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kampuni ya Bima ya Pacis imeonesha kuanza kupata mafanikio makubwa na inaendeshwa kisayansi na kimaadili katika kuwahudumia wateja wake.

Wazo la kuanzisha Kampuni ya Bima lilianza kujitokeza kunako mwaka 1997 na kunako mwaka 2004 Kampuni hii ikasajiliwa nchini Kenya na kuanza kufanya shughuli zake za biashara kunako mwaka 2005. Faida inayopatikana imekuwa ni msaada mkubwa katika huduma kwa Kanisa na Jamii kwa ujumla. Ni matumaini ya Kampuni ya Bima ya Pacis kwamba, wateja wake wataweza kuwa na amani na utulivu baada ya kuwekeza katika Kampuni hii.







All the contents on this site are copyrighted ©.