2013-06-21 11:06:22

Yaliyojiri G8 kwa Mwaka 2013: Biashara, Kodi na Uwazi


Mapambano dhidi ya ukosefu wa fursa za ajira kwa vijana ni kati ya vipaumbele vinavyofanyiwa kazi na wakuu wa G8 mara baada ya kuhitimisha mkutano wake wa Mwaka uliohitimishwa hivi karibuni huko Lough Erne, Ireland ya Kaskazini. Wakuu hawa wameahidi kubana matumizi pamoja na kuendelea kutumia rasilimali na nyenzo zilizopo ili kuhakikisha kwamba, wanatengeneza fursa za ajira kwa vijana.

Wachunguzi wa masuala ya kiuchumi wanabainisha kwamba, hali ya uchumi kwa nchi wanachama wa G8 bado ni mbaya, ingawa hali ya hatari imeondolewa kwa sasa. Sera ya fedha katika nchi wanachama inapaswa kusaidia kuinua hali ya uchumi kwa kusimamia bei ya bidhaa na huduma ndani ya nchi zao; kazi inayotekelezwa na Benki kuu.

Viongozi wa G8 wamekubaliana pia kimsingi kwamba, watalivalia njuga tatizo la ukwepaji kodi na kwamba, wanaendelea kutekeleza mikakati yao ya kiuchumi, kisiasa na kijamii kwa kuongozwa na "T,T,T" yaani, "Trade, Tax and Transparancy" Yaani, Biashara, Kodi na Uwazi na kwamba, watashirikishana taarifa ya mambo ya fedha na kwamba, wameanzisha vita kwa ngazi ya kimataifa dhidi ya "wajanja wachache" wasiotaka kulipa kodi na wale wanaotumia fedha chafu kujijenga kiuchumi na kisiasa.

Mchakato huu unapania kupata fedha ambazo zitatumika kwa ajili ya kuwekeza kwenye medani mbali mbali za maendeleo kama mchakato unaopania kukuza uchumi. Wakuu wa G8 wameelezea kwamba, wataendelea kufanya marekebisho katika mifumo na miundo mbinu ili kufanya maboresho katika hali ya maisha ya raia wao; kuongeza kasi ya ushindani, kutoa mikopo pamoja na kuwajengea uwezo wa mtaji wafanya biashara wadogo wadogo.







All the contents on this site are copyrighted ©.