2013-06-21 07:38:31

Jubilee ni Kipindi cha furaha, shukrani, toba na msamaha!


Askofu Mkuu Josephat Louis Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha anamtakia kheri na baraka Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro, anapoadhimisha Jubilee ya Miaka 25 ya utume wa Kiaskofu. Kilele cha maadhimisho haya ni hapo tarehe 22 Juni 2013 kwenye Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro, iliyoko Jimboni Morogoro. RealAudioMP3

Askofu mkuu Lebulu anasema Jubilee ni kipindi cha furaha, shukrani, toba na msamaha. Askofu Mkude ana kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya maisha lakini zaidi kwa kumteua na kumweka wakfu kushiriki ukuhani wa Kristo katika: kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu.

Ni kipindi cha toba na msamaha: kama binadamu ana karama na mapungufu yake na wala hakuna sababu ya kuona aibu kumwendea Yesu na kuomba msamaha ili kuonja tena upendo na huruma yake sanjari na kumpatia nafasi ya kujazilia pale palipopungua kwa neema na baraka zake. Ukasisi ni dhamana kubwa ambayo Kristo ameikabidhi kwa binadamu mwenye udhaifu, lakini Yeye mwenyewe anafahamu nini cha kutenda.

Askofu Mkuu Lebulu anampongeza Askofu Mkude kwa mchango wake mkubwa si tu katika kuwafundisha, kuwaongoza na kuwatakatifuza Watu wa Mungu Jimbo Katoliki Tanga na Morogoro, lakini pia kwa miaka mingi amekuwa ni Mwenyekiti wa Idara ya Katekesi, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Matunda ya kazi zake ni pamoja na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki kwa lugha ya Kiswahili; Katekisimu ya Kanisa Katoliki, Ufupisho Makini, vitabu ambavyo ni msaada mkubwa kwa maisha ya waamini na wote wenye mapenzi mema wanaozungumza lugha ya Kiswahili.

Jubilee ya Miaka 25 ya Uaskofu ni kipindi maalum kwa Askofu Mkude kumshukuru Mungu akiungana na Familia ya Mungu nchini Tanzania kuendelea kuadhimisha Mwaka wa Imani sanjari na kumbukumbu ya miaka 20 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipochapisha kwa mara ya kwanza Katekesimu Mpya ya Kanisa Katoliki, muhtasari wa: Kanuni ya Imani, Sakramenti za Kanisa, Maisha adili yanayojikita katika kumwilisha Amri za Mungu pamoja na Sala inayomwilishwa katika uhalisia wa maisha ya mwamini.

Askofu mkuu Josephat Lebulu anasema kwamba, kama Makasisi wao ni vyombo mikononi mwa Mwenyezi Mungu anaweza kuwatumikia kadiri ya mpango wake katika maisha na historia ya mwanadamu. Anamwombea Askofu Mkude ili aendelee kuwa ni chombo safi na bora mikononi mwa Mwenyezi Mungu. Awe ni daraja inayowaunganisha watu na Mungu na Mungu na watu. Aendelee kuwaonjesha watu huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya maisha na utume wake kama Askofu. Awe kweli ni kikolezo na chachu ya maendeleo endelevu, daima akipania kuifanya dunia kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.







All the contents on this site are copyrighted ©.