2013-06-21 11:55:52

Askofu mkuu mstaafu Desmond Tutu apongezwa na WCC


Dr. Olav Fyske Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni amempongeza Askofu mkuu mstaafu Desmond Tutu kwa kupewa tuzo la heshima la Templeton, tukio ambalo linatambua mchango wa Askofu mkuu mstaafu Tutu katika kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya matumaini, upatanisho sanjari na kupinga vitendo vya ubaguzi wa rangi vilivyokuwa vinafanyika chini ya utawala wa ubaguzi wa rangi, Afrika ya Kusini.

Dr. Tveit amempongeza Askofu mkuu mstaafuTutu kwa kazi kubwa aliyoifanya wakati wa utume wake Kiongozi mkuu wa Kanisa Afrika ya Kusini, mwanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni na Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Afrika ya Kusini. Askofu mkuu Tutu alipokea tuzo hii hivi karibuni akiwa mjini London. Askofu mkuu mstaafu Tutu alikuwa ni "mwiba" na moto wa kuotea mbali wakati wautawala wa ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini uliokuwa umepamba moto kati ya mwaka 1970 hadi mwaka 1980.

Baada ya kuanguka kwa utawala wa ubaguzi wa rangi, Askofu mkuu mstaafu Desmond Tutu alipewa dhamana ya kuwa ni Mwenyekiti wa Tume ha Ukweli na Upatanisho nchini Afrika ya Kusini iliyoundwa kwenye miaka ya 1990. Tume hii ilisaidia kushinda kinzani, migawanyiko na utengano uliokuwepo miongoni mwa wananchi wa Afrika ya Kusini.

Askofu mkuu mstaafu Desmond Tutu, alisaidia kuendeleza mchakato wa mabadiliko katika demokrasia. Ni kiongozi aliyesimama kulinda na kutetea haki msingi za binadamu; akaongoza mchakato wa majadiliano katika ukweli na uwazi; akapinga ubaguzi wa rangi, fujio na vurugu kwa kukazia umuhimu wa kujenga na kuimarisha majadiliano na umoja, akawa ni mfano wa kuigwa katika kudumisha haki na amani.

Dr. Tveit anasema kwamba, Askofu mkuu Tutu alitetea ile sura na mfano wa Mungu katika maisha ya mwanadamu, akataka kila mtu aheshimiwe na kuthaminiwa si kutokana na rangi yake, bali kwa vile ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Tuzo ya Templeton, ilianzishwa kunako mwaka 1972 na Hayati John Templeton aliyependa tuzo hii itolewe kwa watu watakaochangia kwa kwa njia mbali mbali katika kukuza na kudumisha mwelekeo wa maisha ya kiroho.









All the contents on this site are copyrighted ©.