Vijana wote wanaotaka kushiriki katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani
kwa Mwaka 2013 yanayoongozwa na kauli mbiu “basi enendeni, mkawafanye mataifa yote
kuwa ni wanafunzi” yanayofanyika mjini Rio de Janeiro kuanzia tarehe 23 hadi tarehe
28 Julai kuhakikisha kwamba, wanajiandikisha haraka iwezekanvyo kwani mwisho wa kujiandikisha
ni hapo tarehe 20 Juni 2013, saa 5:59 Usiku kadiri ya saa za Brazil.
Mwaliko huu
pia unatolewa kwa wahusika wote kuhakikisha kwamba, wanakamilisha pia malipo yao katika
siku, ili taratibu nyingine ziweze kuendelea kutekelezwa kwani hili ni tukio linalotarajiwa
kuwakusanya makundi makubwa ya vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia.
Ni
jambo la muhimu sana vijana kujisajili ili waweze kuwa ni sehemu ya wale watakaoshiriki
rasmi katika Maadhimisho haya, jambo litakaloliwezesha Baraza la Maaskofu Katoliki
Brazil kuweza kujipanga kuhusu: malazi, chakula na usafiri. Kimsingi ni tukio linalowashirikisha
vijana na watu wote wenye mapenzi mema, lakini kutakuwepo na maeneo maalum ambayo
wataingia wale tu wenye vitambulisho maalum kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana
Duniani kwa Mwaka 2013.
Makundi ya vijana yafanye mipango yake kwa njia ya
wakuu wa makundi haya, lakini hata vijana wenye uwezo na jeuri yao wanaweza kushiriki
bila wasi wasi wowote. Gharama ya kila mtu anayeomba kushiriki katika Maadhimisho
haya ni kuanzia dolla za kimarekani 300 na kiwango cha chini kabisa ni dolla 250.