2013-06-20 11:19:13

Saidieni Familia za Wakimbizi, ili waonje upendo na ukarimu wenu!


Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 20 Juni inaadhimisha Siku ya Wakimbizi Duniani. Baba Mtakatifu Francisko anasema, Wakimbizi na Familia zao wanapaswa kusaidiwa kwa hali na mali na kwamba, kila hatua ya maisha ya binadamu inapaswa kulindwa, kutunzwa na kuheshimiwa.

Baba Mtakatifu Francisko ameyasema hayo wakati wa Katekesi yake, Jumatano, tarehe 19 Juni 2013 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, uliokuwa umefurika kwa umati mkubwa wa waamini, mahujaji na watu wenye mapenzi mema.

Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, kuna wakati ambapo wakimbizi wanalazimika kuzikimbia nchi zao kwa kuacha kila kitu ili kuokoa maisha yao. Madhulumu, ubaguzi, maafa asilia na vita ni kati ya mambo ambayo yanapelekea watu wengi kuzikimbia nchi zao.

Hata katika mazingira kama haya, bado familia zinaweza kujikuta zikiwa zimetengana sanjari na kukabiliwa na hali ngumu zaidi ya maisha, changamoto kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwaonjesha mshikamano wa upendo kwa kuwahudumia, kwani wao ni kielelezo cha uso wa Kristo Mteswa!

Baba Mtakatifu akiwa bado na kumbu kumbu ya Maadhimisho ya Injili ya Uhai kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai katika hatua zake zote kadiri ya mpango wa Mungu. Waamini wawe ni mashahidi wanaoipokea Injili ya Uhai, Waishuhudie na kuitangaza hadi miisho ya dunia, kwani kila Mkristo anadhamana ya kuikumbatia Injili ya Uhai.

Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa linabainisha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni 45 waliolazimika kuyakimbia makazi na nchi zao, sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.