Vyombo vya habari vina dhamana ya kulinda na kukoleza misingi ya haki, amani na maendeleo
endelevu!
Vyombo vya upashanaji habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Wakristo Mashariki ya
kati havina budi kujielekeza zaidi katika huduma inayopania kuendeleza mchakato wa
haki na amani na kama kielelezo cha mshikamano wa upendo na wote wanaoteseka kutokana
na kinzani za kisiasa, kijamii na kidini huko Mashariki ya Kati.
Mama Kanisa
anaendelea kuwahamasisha Wakristo na watu wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanalisaidia
Kanisa huko Mashariki ya Kati kukuza na kudumisha misingi ya haki na amani. Haya ni
kati ya mawazo makuu yaliyojitokeza katika tamko la pamoja mara baada ya kuhitimisha
semina iliyojadili kuhusu mchango wa vyombo vya habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa
na Kanisa huko Mashariki ya Kati katika mchakato wa kudumisha haki na amani.
Semina
hii imehudhuriwa na viongozi wakuu wa Kanisa, Serikali na wadau katika sekta ya mawasiliano
ya kijamii. Kwa pamoja wanasema, kuna haja kwa vyombo vya habari kulinda na kudumisha
tunu za haki msingi za binadamu, amani kwa kuangalia mambo ambayo yanawagawa watu
ili kuweza kutafuta ufumbuzi wa kudumu. Vyombo vya habari vijikite zaidi katika mchakato
wa kudumisha haki, amani, upendo na mshikamano kati ya watu badala ya kuchochea vurugu
na kinzani.
Wajumbe wanasema, vyombo vya habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa
na Kanisa vinaweza kusaidia kutunza na kuimarisha utambulisho wake, visipokuwa makini
vinaweza kutumiwa na wanasiasa kwa masilahi yao binafsi, hapo utakuwa ni mwanzo wa
kufilisika kwa vyombo hivi. Vyombo hivi huko Mashariki ya Kati vina dhamana nyeti
ya kulinda na kutetea haki msingi za binadamu. Viwe ni jukwaa la majadiliano ya kidini
na kiekumene na kwamba, kuna haja ya kuwa na ushirikiano wa karibu na Baraza la Kipapa
la Mawasiliano ya Jamii katika kuchapisha vitabu na majarida mbali mbali.
Vyombo
hivi viwe ni vielelezo vya msingi wa maadili na utu wema; mahali ambapo vijana wa
kizazi kipya watajifunza tunu msingi za maisha ya kijamii; ili waweze kuufahamu na
kuupenda ukweli; wasimame kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha; wawe ni mashahidi
wa uzuri na wema unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kama anavyosema Baba Mtakatifu
Francisko.
Ni mwaliko kwa nchi zilizoko Mashariki ya Kati kusitisha vita na
kinzani ambazo zimekuwa ni chanzo kikuu cha vifo na hali ngumu ya maisha na badala
yake waanze mchakato wa kutetea, kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo
na mshikamano wa kitaifa na kimataifa!
Hii iwe ni fursa ya kuendeleza majadiliano
ya kidugu baina ya waamini wa dini na madhehebu mbali mbali, daima wakitafuta umoja
wa kitaifa na mafao ya wengi. Watu wajifunze kuheshimiana na kuthaminiana ili kuondokana
na sera tenge za kiubaguzi kwa misingi ya kidini.