Uingereza imeahidi kuzijengea uwezo nchi zinazoendelea ili ziweze kutambua thamani
ya maliasili zake kwa kuwataka wawekezaji katika nchi hizo kulipa kodi inayostahili,
kuweka uwazi katika mapato yanayotokana na maliasili hizo na kuweza kuthaminisha ardhi
ya nchi hizo kwa manufaa zaidi. Aidha, Uingereza inataka nchi zinazoendelea kutokuwauzia
wawekezaji ardhi bali ziwe na uwezo wa kutumia ardhi yake na kuithaminisha kama kitega
uchumi chake kwa manufaaa zaidi.
Msimamo huo wa Uingereza ulielezwa na Waziri
Mkuu wa Uingereza, Mheshimiwa David Cameron katika mkutano wa viongozi wachache wa
Afrika ambao wamekuwa wanakutana na Waziri Mkuu huyu kumweleza matakwa ya Afrika ambayo
yatawasilishwa katika Mkutano wa Viongozi Nchi Tajiri na Zenye Viwanda Vingi Zaidi
Duniani (G-8) ulioanza Ireland ya Kaskazini Jumatatu, Juni 17, 2013 na unaofanyika
kwa siku mbili.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania alikuwa miongoni mwa
viongozi hao wachache wa Afrika waliokutana na Waziri Mkuu Cameron ambaye pia ametaka
Serikali za nchi zinazoendelea kuonyesha uwajibikaji mkubwa zaidi na uwazi zaidi katika
matumizi na mapato ya kodi yanayotokana na maliasili hizo.
Uingereza ndiye
mwenyekiti wa G8 mwaka huu na imeliweka suala la biashara, kodi na uwazi katika uwekezaji
na biashara kama moja ya agenda yake katika kuzisaidia nchi zinazoendelea. Nchi hiyo
ndiyo itawakilisha mawazo na maoni ya Afrika kwenye Mkutano huo wa viongozi wa G-8.
Katika mpango huo, Uingereza inataka kuzishawishi nchi za G8 kusaidia nchi
zinazoendelea kujenga uwezo wa kutambua mali asili zilizopo, kutambua thamani yake,
kodi inayolipwa na kama inastahili na kuzitaka kampuni zinazowekeza kuwa wazi zaidi
katika biashara zao na shughuli wanazofanya ili nchi na watu wake ziweze kufaidika
na mali asili yake. Nchi wanachama wa G8 ni Canada, Ufaransa, Ujerumani, Italia, Japan,Urusi,
Marekani na Uingereza.
Mbali na mkutano huo wa baadhi ya nchi za Afrika na
Bw. Cameron, Rais Kikwete amekutana na kufanya mazungumzo na Sir. Richard Branson,
mfanyabiashara mkubwa na bilionea wa Uingereza ambaye ni mwenyekiti wa Kundi la Makampuni
ya Virgin yanayoendesha shughuli mbali mbali ukiwamo usafiri wa anga na reli.
Rais
amefanya mazungumzo na Bw. Branson kwa nia ya kumshawishi kuwekeza Tanzania katika
masuala ya anga, kupitia kampuni yake ya Virgin Atlantic Airways ambapo Bw. Branson
ameahidi kufanyia utafiti suala hilo lakini pia ameonyesha nia ya kuwekeza kwenye
reli. Rais Kikwete pia ametembelea makao makuu na uwanja wa timu ya soka la Sunderland
na kujionea jinsi vijana wadogo wanavyopata mafunzo na kuendeleza vipaji vyao vya
mpira.
Kampuni ya umeme ya Symbion imeahidi kujenga shule ya kufundishia na
kuendeleza vipaji vya mpira kwa vijana wadogo ambapo timu ya Sunderland imeahidi kutoa
mafunzo, walimu na kujenga uwezo kwa watanzania.