Hotuba ya mhe. Sophia M. Simba (mb), Waziri wa maendeleo ya jamii, jinsia na watoto
wakati akizindua rasmi mtandao wa mawasiliano ya simu wa kusaidia watoto hapa nchini
(Tanzanian child helpline) tarehe 16 Juni, 2013.
Kwanza, napenda kuchukua
nafasi hii kumshukuru mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha sote kukutana
hapa ili kuweza kushuhudia tukio hili muhimu katika kuwezesha watoto kupata mojawapo
ya haki yao ya msingi.
Ndugu Wageni Waalikwa
Mnamo mwaka 2009 Wizara
ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa masuala
ya watoto hapa nchini ilifanya utafiti wa kina ili kufahamu ukubwa na sura ya ukatili
wa kijinsia, kimwili na kiakili yanayowasibu wasichana na wavulana hapa nchini.
Utafiti
huu ulifanywa na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Afya ya Sayansi na Tiba cha Muhimbili
(Muhimbili University of Health and Allied Sciences – MUHAS) kwa kushirikiana na UNICEF
na Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Center for Diseases Control – CDC). Ripoti
ya Utafiti huu ilizinduliwa rasmi mnamo tarehe 09 Agosti, 2011 na aliyekuwa Naibu
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa bibi Asha-Rose Migiro.
Matokeo ya utafiti huu
yalionyesha kuwa kuna kiwango kikubwa cha ukatili dhidi ya watoto na matukio mengi
ya ukatili kwa watoto yamekuwa yakifanyika ama shuleni na au nyumbani. Hali hii ilipelekea
wadau wa masuala ya watoto (Taasisi za serikali na zile zisizokuwa za serikali) kuandaa
Mpango Mkakati wa mwaka mmoja wa Kushughulikia Tatizo la Ukatili Dhidi ya Watoto (2012
– 2013) na hatimaye kuandaa Mpango wa miaka mitatu wa kushughulikia tatizo hilo (2013
– 2016) ambao ulizinduliwa mwezi April mwaka huu.
Ndugu Wageni Waalikwa.
Mnamo
tarehe 3 Januari, 2013 Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto iliingia makubaliano
na Asasi Isiyokuwa ya Kiserikali ya C-Sema kuhusu uendeshaji wa mtandao huu katika
maeneo ya majaribio (Pilot Areas). Uendeshaji wa mtandao huu katika maeneo haya utasaidia
kutoa picha halisi ya namna nzuri ya uendeshaji wa mtandao wa namna hii hapa nchini.
Mtandao huu utafanya kazi katika Wilaya/ Manispaa za Temeke, Magu, Bukoba Vijijini,
Musoma Mjini, Kasulu na Hai ambapo muda si mrefu utaanza kufanya kazi katika Manispaa
za Ilala na Kinondoni. Lengo kuu la Serikali kwa kushirikiana na wadau wake wa maendeleo
ya watoto ni kuhakikisha kuwa mtandao huu unafanya kazi katika maeneo yote ya Tanzania
Bara.
Ndugu Wageni Waalikwa Uanzishaji wa Mtandao wa Mawasiliano wa Kusaidia
Watoto ni moja wapo ya shughuli ambazo zilipangwa kutekelezwa na Wizara yangu katika
Mpango wa Miaka Mitatu wa Kushughulikia Ukatili Dhidi ya Watoto uliozinduliwa hivi
karibuni. Kadhalika, ni moja wapo ya utekelezaji wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa
Haki za Watoto (The UN Convention on the Rights of the Child – UN CRC) ambao nchi
yetu iliusaini na kuuridhia mara baada ya kupitishwa kwake.
Mtandao huu utatoa
fursa kwa watoto na au watu wazima kwa niaba ya watoto kutoa taarifa za ukatili unaofanywa
kwa watoto katika eneo fulani ili kuwezesha wahusika kufuatilia kwa karibu na urahisi
kwa ajili ya kutoa msaada kwa mtoto/watoto waliofanyiwa vitendo vya ukatili na kumchukulia/kuwachukulia
hatua mhusika/wahusika wa vitendo hivyo vya ukatili.
Kwa kiasi kikubwa kama
mtandao utatumiwa kwa malengo haya, ni imani yangu kuwa itasaidia kupunguza ukatili
dhidi ya watoto na vile vile kuhakikisha kuwa watoto wanapata msaada stahiki kwa wakati.
Ndugu
Wageni Waalikwa Ni matumaini ya Wizara yangu kuwa wadau mbalimbali watajitokeza
kushirikiana nasi katika kuhakikisha kuwa huduma hii inapatikana katika maeneo yote
hapa nchini katika muda muafaka ili kuhakikisha kuwa watoto wetu wanapata ulinzi wa
kutosha.
Kadhalika, ni matumaini yangu kuwa jamii na wahusika wote watawezeshwa
kupata uelewa wa kutosha kuhusu matumizi sahihi ya mtandao huu.
Mwisho, napenda
pia kuchukua fursa hii rasmi kutamka kuwa nimezindua rasmi mtandao wa mawasiliano
ya simu wa kusaidia watoto katika maeneo ya majaribio niliyoyataja hapo mwanzo.
Tuungane
kwa Pamoja Kuijenga Tanzania Imfaayo Mtoto.