2013-06-17 09:18:14

Maadhimisho ya Mtoto wa Afrika yakoleze mapambano dhidi ya mila na desturi zilizopitwa na wakati!


Shirika la kuhudumiwa watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF katika Maadhimisho ya Mtoto wa Afrika yaliyofikia kilele chake hapo tarehe 16 Juni 2013, linasema kwamba, kuna nchi kumi Barani Afrika ambazo bado kiwango cha vifo vya watoto wenye umri chini ya miaka mitano kiko juu zaidi. Nchi hizi ni pamoja Sierra Leone, Mali, Chad, DRC, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, Guinea Bissau, Angola, Burkina Faso na Burundi.

UNICEF inapenda kushirikiana kwa karibu zaidi na Umoja wa Afrika ili kuhakikisha kwamba, mila zote zenye kuleta madhara kwa watoto zinaondolewa kwani hili ni jukumu la kila mmoja. Itakumbukwa kwamba, hii ndiyo kauli mbiu ambayo imeongoza pia Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika kwa Mwaka 2013.

Familia na Jamii kwa ujumla ni msingi wa ustawi, maendeleo na afya bora kwa watoto Barani Afrika. Kuna haja ya kuhakikisha kwamba, mila za ukeketaji kwa watoto wa kike zinapigwa marufu. Bado kuna ndoa za utotoni katika baadhi ya nchi za Kiafrika vitendo vinavyodumaza maisha ya watoto wengi.

Kati ya mambo yanayopaswa pia kuvaliwa njuga UNICEF inasema, ni watoto kuhusishwa na imani za kishirikina jambo ambalo limepelekea watoto wengi kutolewa sadaka kwa kudhani kwamba, ni chambo cha fedha, utajiri na madaraka. Ni katika mwelekeo kama huu, watoto na watu wenye ulemavu wa ngozi wamejikuta wakidhulumiwa katika Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.