2013-06-17 07:35:03

Dini zinawajibu wa kudumisha na kutetea utu na heshima ya binadamu!


Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini, Jumamosi jioni tarehe 15 Juni 2013 ameshiriki katika Ibada ya Masifu ya Jioni kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Ceadda, London, Uingereza. Amekazia umuhimu wa kulinda. Kudumisha na kutetea utu na heshima ya kila mtu kama kielelezo makini cha ujenzi wa misingi ya haki na amani duniani.

Kardinali Tauran ameyasema haya wakati wa ziara yake ya kichungaji nchini Uingereza kama sehemu ya mchakato unaopania kujenga na kuimarisha urafiki kati ya waamini wa dini mbali mbali duniani, ziara ambayo ilianza rasmi hapo tarehe 12 na kuhitimishwa hapo tarehe 16 Juni 2013.

Akiwa mjini London, Kardinali Tauran amekuta na kuzungumza na waamini wa dini mbali mbali nchini Uingereza pamoja na kushiriki sala kwa ajili ya kuombea misingi ya haki na amani, iliyowashirikisha waamini wa dini mbali mbali duniani. Katika mahubiri na hotuba zake, amekazia umuhimu wa kujenga na kuimarisha amani.

Wakati wa machafuko, kinzani na migogoro mambo ambayo yanapelekea kuvunjika kwa misingi ya amani, watu wengi wanajikuta wakiteseka na kuhangaika kutokana na baadhi ya watu kutafuta masilahi yao binafsi badala ya kuchuchumilia mafao na ustawi wa Jamii inayohusika. Kutokana na kuwepo kwa wasi wasi wa kutokomea kwa misingi ya amani, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuendelea kuzungumzia suala hili, na kila mmoja ajitahidi kuwa kweli ni chombo cha amani pamoja na kushikamana na watu wengine kwa ajili ya mafao ya wengi.

Kardinali Tauran anasema kwamba, dhana ya jirani imekuwa na kupanuka kutokana na utandawazi na mwingiliano wa watu wanaohama kutoka sehemu moja hadi nyingine. Hawa ni watu wenye imani, tamaduni na asili tofauti; kimsingi ndio wanaounda kundi la majirani, changamoto ya kujenga urafiki na wote; kwa kuheshimiana na kuthaminiana; kwa kushirikiana pamoja na kusimama kidete kulinda na kutetea haki na mafao ya wengi; amani na utulivu pamoja na maendeleo endelevu.

Waamini wa dini mbali mbali wanapaswa kushirikiana katika kuenzi tunu msingi za maisha ya kijamii kama nguzo za ujenzi wa amani.









All the contents on this site are copyrighted ©.