2013-06-15 11:41:50

Wakristo wanahamasishwa kuwa ni wajumbe wa amani na upatanisho kati ya Mungu na mwanadamu!


Maisha ya Kikristo si mwaliko kwa waamini kujitafuta na kujitafutia amani yao binafsi, bali wanatumwa na Kristo kwenda hadi miisho ya dunia kutangaza Habari Njema ya Wokovu na kwamba, Yesu amejinyenyekesha ili aweze kuwa ni daraja ya upatanisho kati ya Mungu na mwanadamu.

Yesu Kristo ameonesha utii, hata akahesabiwa kuwa ni kati ya wadhambi ili kumpatanisha mwanadamu na Mwenyezi Mungu, changamoto na mwaliko kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanajipatanisha na Mungu kama wanavyohamasishwa na Mtakatifu Petro katika Waraka wake kwa Wakorintho. Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko Jumamosi, tarehe 15 Juni 2013 wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, kilichoko mjini Vatican.

Upatanisho ni mchakato ambao umemfanya Yesu Kristo kujitwika dhambi za binadamu, ili aweze kuwapatanisha na Mwenyezi Mungu na hivyo kuwajalia Sakramenti ya Upatanisho inayomwonjesha mwamini huruma na upendo wa Mungu katika maisha yake. Waamini wanapomuungamia Yesu dhambi zao, anawasamehe na kuwapatia mwelekeo mpya wa maisha kwani hii ni sehemu ya utume wake hapa duniani, uliopelekea hata akateswa, kufa na kufufuka kutoka katika wafu. Waamini waonje na kuguswa na upendo wa Kristo ndani mwao!

Baba Mtakatifu anasema, amani mintarafu Mafundisho ya Kristo ni mchakato unaowasukuma waamini kupeleka ujumbe wa upatanisho kati ya Mungu na binadamu hadi miisho ya dunia, huku wakihamasishwa na utume huu ambao wamekabidhiwa na Kristo mwenyewe na kiini cha utume wao! Waamini wanapaswa kulifahamu Fumbo la Msalaba katika maisha yao, Msalaba ambao ni matokeo ya dhambi na uasi wa binadamu.

Huu ni ukweli unaofumbatwa katika Fumbo la Msalaba, pale ambapo moyo wa Yesu Kristo ulipotobolewa kwa mkuki, humo yakatoka maji na damu; kielelezo cha Sakramenti za Kanisa. Hapa ni mahali ambapo hekima ya Kikristo ikabubujika na kwamba, amani ya kikristo inafumbatwa katika uhalisia wa maisha na kwamba, upendo wa Kristo unawawajibisha kutangaza ujumbe wa amani na upatanisho miongoni mwa watu!







All the contents on this site are copyrighted ©.