Sinodi za Maaskofu ni chombo makini katika maisha na utume wa Kanisa
Baba Mtakatifu Francisko kwa mara ya kwanza, Alhamisi, tarehe 13 Juni 2013 amekutana
na kuzungumza na wajumbe wa Sekretarieti ya Sinodi ya Kumi na tatu ya Maaskofu, kwa
kutambua na kuthamini umuhimu wa Sinodi katika maisha na utume wa Kanisa; dhamana
inayohitaji utayari, uwajibikaji na sadaka ambayo wakati mwingine inawalazimisha kusafiri
umbali mrefu.
Baba Mtakatifu amekazia umuhimu wa mchakato wa Uinjilishaji
Mpya unaopania kutangaza imani ya Kikristo na kwamba, hii ndiyo dhamana ya Kanisa
kwa ujumla, hususan katika nchi ambazo zilibahatika kusikia Injili ya Kristo lakini
kwa sasa zimemezwa na malimwengu. Waamini katika nchi hizi wanapaswa kutangaziwa Injili
ili waweze kukutana tena na Kristo anayewakirimia mabadiliko mapya katika hija ya
maisha yao ya ndani kabisa. Hii ni changamoto ya mikakati ya kichungaji.
Baba
Mtakatifu anabainisha kwamba, kuna haja ya kuibua mbinu na mikakati mipya kutokana
na mabadiliko yanayoendelea kujitokeza kwenye Jamii nyingi pamoja na kupambanua mbinu
ambazo Mama Kanisa anaweza kuzitumia ili kufikisha ujumbe wa Injili ya Kristo kwa
watu nyakati hizi sanjari na kupata majibu makini ya masuala yanayomtatiza binadamu
ili kuimarisha mshikamano wa dhati, kama alivyowahi kubainisha Mtumishi wa Mungu Papa
Paulo wa sita.
Dhamana ya Uinjilishaji si tu kwa ajili ya Wakristo bali ni
kwa ajili ya binadamu wote, changamoto anasema Baba Mtakatifu Francisko kwa waamini
wote kujisikia kuwa ni wadau wa Uinjilishaji Mpya, na kamwe wasiogope kutoka katika
ubinafsi wao huku wakijiaminisha kwa huruma na upendo wa Mungu unaowaongoza, bila
kusahau kwamba, Mwinjilishaji Mkuu ni Roho Mtakatifu anayesaidiwa na vyombo mbali
mbali vya mawasiliano ya jamii.
Waamini wanapaswa kumwachia nafasi Roho Mtakatifu
awasaidie kutoa ushuhuda wa Injili unaomwilishwa kwa njia ya matendo, moyo wa sala,
upendo kwa wote, lakini zaidi kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii;
Unyenyekevu na moyo wa kiasi na zaidi sana, utakatifu wa maisha! Kwa njia hii, Uinjilishaji
utaweza kuzaa matunda yanayokusudiwa!
Baba Mtakatifu Francisko anakiri kwamba,
Sinodi za Maaskofu ni kati ya matunda ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na kwamba,
katika kipindi cha miaka hamsini, zimekuwa na mchango mkubwa sana katika maisha na
utume wa Kanisa kwa kukazia umoja na mshikamano miongoni mwa Maaskofu, hali ambayo
ameishuhudia mwenyewe wakati alipokuwa anahudhuria Sinodi mbali mbali. Ni matumaini
ya Baba Mtakatifu kwamba, Sinodi za Maaskofu zitaendelea kuboreshwa ili kuimarisha
majadiliano na ushirikiano miongoni mwa Maaskofu na Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Baba
Mtakatifu amewashukuru wajumbe kwa mkutano wao uliomsaidia kuweza kubaini tema itakayoongoza
Sinodi nyingine tena ya Maaskofu. Amewashukuru wote kwa moyo wa ukarimu, utayari na
ushirikiano waliomwonesha na kwamba, kazi hii kwa wakati muafaka itaweza kuzaa matunda
ajaa kwani Yesu Kristo ni njia, ukweli na uzima kwa kila mtu na kila mmoja wao.