2013-06-13 15:20:20

Simameni kidete kulinda, kutetea na kuendeleza misingi ya haki, amani na mshikamano!


Kardinali Jean Lous Tauran wakati wa ziara yake ya kikazi nchini Uingereza, siku ya Alhamisi tarehe 13 Juni 2013 alitembelea Seminari ya dini ya Kihindu. Katika hotuba yake amekazia kwa namna ya pekee, ushirikiano unaopaswa kujengeka kati ya waamini wa Kanisa Katoliki na Wahindu katika kujenga na kuimarisha utamaduni wa kujali kama msingi wa ujenzi wa amani. Kanisa Katoliki linapania kuendeleza ushirikiano na waamini wa dini ya Kihindu mahali popote pale walipo.

Katika ulimwengu wa utandawazi, mapokeo ya dini nyingi yanaonekana kana kwamba, yamepotea na kumezwa na malimwengu. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican miaka hamsini iliyopita, walikazia umuhimu wa majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali duniani; changamoto hii inapaswa kufanyiwa kazi hasa wakati huu ambapo kuna mwingiliano mkubwa wa watu wenye dini na tamaduni mbali mbali.

Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba yake alipokutana kwa mara ya kwanza na wawakilishi wa dini na madhehebu mbali mbali waliokuwa wamehudhuria Ibada ya Misa Takatifu wakati alipokuwa anasimikwa kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, alisema, Kanisa Katoliki linatambua umuhimu wa kudumisha urafiki, heshima miongoni mwa Jamii ya watu wenye dini na mapokeo mbali mbali ni dhamana ambayo imeendelezwa kwa namna ya pekee na Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini tangu lilipoanzishwa.

Hii ni changamoto kwa waamini kujitahidi kufahamu imani ya jirani zao; waguswe na hekima na wema unaopatikana kwenye dini hizi sanjari na kuunda mazingira yatakayowawezesha watu wote kuishi kwa amani, uhuru na utulivu. Mchakato huu uwasaidie waamini wa dini mbali mbali kuwa kweli ni wachamungu. Huruma ni fadhila inayopatikana katika dini mbali mbali duniani kama ilivyobainishwa katika Vitabu Vitakatifu, kiasi cha kuwawezesha watu kama akina Mahatima Ghandi wakasimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki na amani.

Kardinali Tauran anasema fadhila ya huruma iwasaidie waamini kuguswa na mateso ya jirani zao, kiasi cha kushiriki kuleta mabadiliko katika ulimwengu mamboleo, kama alivyofanya yule Msamaria mwema anayesimuliwa katika Maandiko Matakatifu. Baba Mtakatifu Francisko katika utume wake anaendelea kuwahamasisha wakristo na watu wote wenye mapenzi mema kuonesha mshikamano wa dhati na maskini na wote wanaoteseka sehemu mbali mbali za dunia.

Athari za myumbo wa uchumi kimataifa zinaendelea kuonesha umuhimu kwa Jamii kushirikiana na kushikamana ili kwa pamoja waweze kukabiliana na changamoto hizi, kwa kulinda na kudumisha misingi ya haki na amani, licha ya tofauti za kiimani. Lakini anasema Kardinali Tauran fadhila ya huruma inawaunganisha wote mintarafu Mapokeo ya dini zao, changamoto na mwaliko wa kukua na kukomaa katika maelewano, kwa kuheshimiana na kuthaminiana, ili kwa pamoja waweze kusimama kidete kulinda, kutetea na kuendeleza misingi ya: haki, amani na mshikamano.







All the contents on this site are copyrighted ©.