Vatican na Cape Verde watiliana sahihi mkataba wa ushirikiano
Jamhuri ya wananchi wa Cape Verde na Vatican, Jumatatu tarehe 10 Juni 2013 imetiliana
sahihi mkataba wa uhusiano unaolitambua Kanisa Katoliki kisheria. Waziri mkuu wa Cape
Verde Bwana Josè Maria Neves ameongoza ujumbe wa Serikali ya Cape Verde na Askofu
mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa
mjini Vatican ameongoza ujumbe wa Vatican.
Kwa muda wa miaka 37, Cape Verde
imekuwa na uhusiano mwema na Vatican, jambo ambalo limepelekea hata kufikia uamuzi
wa kulitambua Kanisa kisheria katika masuala ya: ndoa, maeneo ya ibada, taasisi za
elimu na afya zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki nchini humo; ufundishaji
wa elimu ya dini shuleni; huduma za maendeleo jamii pamoja na huduma za maisha ya
kiroho kwa vikosi vya ulinzi na usalama pamoja na huduma ya kiroho kwenye magereza.
Itifaki hii inatarajiwa kuanza kutumika rasmi baada ya siku 30 tangu pande hizi mbili
zilipobadilishana mikataba hii.