Kongamano la Utoto Mtakatifu Jimbo kuu la Dar es Salaam katika Maadhimisho ya Mwaka
wa Imani!
Jimbo kuu la Dar es Salaam kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 17 Juni 2013 litakuwa na
Kongamano la Utoto Mtakatifu, linalofanyika Jimboni Ifakara na linaloongozwa na kauli
mbiu "Mtoto ni Imani". Kongamano hili linafanyika wakati ambapo Mama Kanisa anaendelea
kuadhimisha Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto
wa kumi na sita.
Wanachama
wa Utoto Mtakatifu kutoka katika Majimbo yanayounda Jimbo kuu la Dar es Salaam, pamoja
na mambo mengine watachambua kuhusu"Mtoto na Mwaka wa Imani; Malezi ya Mtoto na changamoto
za utandawazi. Wazazi na walezi wa Utoto Mtakatifu Jimbo kuu la Dar es Salaam, wao
watashirikishwa kuhusu umuhimu wa walezi katika maisha ya imani na mfano wa maisha
ya Kikristo.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican, ikihojiana na Askofu mkuu
Protase Rugambwa, Katibu mkuu mwambata na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya Kazi za Kimissionari
anapenda kukazia kwamba, malezi ya watoto yanapaswa kupata chimbuko lake katika familia.
Wazazi wawasaidie watoto wao kufahamu tunu msingi za maisha ya Kikristo na kiutu na
kijamii, wakitambua kwamba, wao ndio makatekista na walimu wa kwanza kwa maisha ya
watoto wao.
Askofu mkuu Rugambwa anaendelea kusema kuwa utume wa Utoto Mtakatifu
unaopewa kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wa Kanisa nchini Tanzania hauna
budi kwenda sanjari na dhamana na wajibu wa wazazi na walezi katika malezi na makuzi
ya watoto: kiimani, kimaadili na kiutu. Wazazi na walezi wawashirikishe watoto wao
katika maisha na utume wa Kanisa. Watambue na kuthamini maisha ya familia inayoanza
pale nyumbani, inakua na kupanuka katika Kigango, Parokia, Jimbo na Kanisa lote katika
ujumla wake.
Watoto wafahamishwe umuhimu wa familia na dhamana yake, ili wawe
tayari kwa siku za usoni kuisimamia, kuilinda na kuitetea. Wazazi waendelee kushirikiana
na Kanisa katika malezi na makuzi ya watoto na kwamba, Utoto Mtakatifu upate chimbuko
lake katika Familia na kuendelea kupanuka ili kujenga na kuimarisha Familia ya Mungu
inayowajibika katika Kanisa mahalia na katika Kanisa la kiulimwengu.