2013-06-12 14:38:31

Kanisa ni mahali pa kuonja upendo, huruma na matumaini kutoka kwa Mwenyezi Mungu!


Baba Mtakatifu Francisko katika mwendelezo wa Katekesi kuhusu Kanuni ya Imani kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Jumatano tarehe 12 Juni 2013 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, ameendelea kupembua kuhusu Kanisa kama Familia ya Mungu inayoitwa kuishi maisha mapya katika Kristo. Waamini wanashirikishwa katika Familia hii kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, wanamozaliwa kwa Maji na Roho Mtakatifu, changamoto ya kumwilisha amri ya upendo kwa Mungu na jirani.

Baba Mtakatifu anawakumbusha Wakristo kwamba, wanayo dhamana inayowataka kuwa ni chachu ya matumaini ya upendo ulimwenguni ambako watu wamejeruhiwa kwa dhambi na uovu. Licha ya giza linalowazunguka wanadamu katika maisha haya, lakini waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee kuwa ni mwanga unaoonesha matumaini ya kesho iliyo bora zaidi.

Baba Mtakatifu anasema, wema wa Mwenyezi Mungu una nguvu kubwa zaidi kuliko maovu yanayojionesha ulimwenguni. Hatima ya maisha ya mwamini ni Ufalme wa Mungu ulioanzishwa hapa duniani na Yesu Kristo, utakaofikia utimilifu wake kwa kushiriki furaha ya uzima wa milele mbinguni. Hii ndiyo maana ya Kanisa kuwa ni Familia ya Mungu, kielelezo makini cha mpango wa upendo wa Mungu kwa Familia ya binadamu.

Mwishoni, Baba Mtakatifu anaomba ili Kanisa daima liwe ni mahali ambapo kila mtu anaweza kuonja huruma ya Mungu, kwa: kukaribishwa, kupendwa, kusamehewa pamoja na kuhamasishwa kuishi vyema mintarafu misingi ya Injili.

Akizungumza na waamini pamoja na mahujaji kwa lugha mbali mbali, Baba Mtakatifu anawataka waamini kuwa ni vyombo vya upendo na huruma ya Mungu kwa watu wake; waendelee kumpenda Kristo na Kanisa lake kwa njia ya ushuhuda makini wa maisha ya Kiinjili. Waamini wajenge ndani mwao ujasiri na uthabiti wa imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.