2013-06-11 10:32:25

Jitokezeni kimasomaso kutangaza Injili ya Kristo bila ya kujibakiza! Mmepewa bure, toeni bure!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumanne, tarehe 11 Juni 2013 ameadhimisha Siku kuu ya Mtume Barnaba aliyejitosa kimasomaso kuhubiri Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia kwa njia ya maneno lakini hasa zaidi kwa matendo yake. Ibada ya Misa takatifu imefanyika kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, kilichoko mjini Vatican.

Hii ndiyo chemchemi ya furaha waliyokuwa nayo waamini wa Kanisa la Mwanzo, kiasi kwamba, waliweza kuchangia kwa hali na mali kufanikisha jitihada za Uinjilishaji, kwa kutambua kwamba, yote waliyokuwa nayo wamepata bure na kwa njia hii wanapaswa kuyatumia kwa ajili ya ustawi na mafao ya Kanisa kwa ujumla.

Baba Mtakatifu anasema, wafuasi wa Kristo wanaojitosa kikweli kweli kutangaza Injili ya Kristo hawana budi kuchuchumilia fadhila ya ufukara; kwa kuutolea ushuhuda wa uwepo wa Mungu anayewawezesha katika yote. Kanisa linapaswa kuonesha ile taswira ya ufukara kwa kutumia vyema rasilimali yake kwa ajili ya mafao, ustawi na maendeleo ya wengi.

Kanisa lijiepushe anasema Baba Mtakatifu kuwekeza katika mambo ya kidunia kama wafanyavyo wafanyabiashara wanaotafuta mali na faida kubwa! Vitegauchumi vya Kanisa viwe ni kwa ajili ya huduma na maendeleo kwa binadamu.

Hiki ndicho kielelezo cha maisha kilichotolewa na Mitume na Wafuasi wa Yesu; kwa njia ya ufukara wao, wakawa tayari kujitosa kutangaza matendo makuu ya Mungu. Bila majitoleo ya wafuasi wa Kristo, Kanisa litadumaa na kusinyaa! Changamoto kwa waamini kujitoa kwa ajili ya Kanisa, kwani wamepewa yote bure na kwamba, wao ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.