2013-06-10 09:41:42

Mshikamano kati ya Vatican na Serikali ya Italia kwa ajili ya majadiliano ya kidini na mafao ya wengi!


Uhusiano wa dhati kati ya Vatican na Serikali ya Italia ni jambo msingi ambalo limemwilishwa katika taasisi na kuota mizizi yake katika historia sanjari na kukuzwa katika majadiliano ya kidini. Sehemu ya hotuba iliyotolewa na Rais Giorgio Napolitano wa Italia alipokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican, kama kielelezo cha mshikamano kati ya Serikali na Wananchi wa Italia kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro.


Rais Napolitano anasema kwamba, wakati Baba Mtakatifu Francisko alipokuwa anaanza utume wake kama Kahlifa wa Mtakatifu Petro, alikuwepo kushuhudia tukio hili la kihistoria, hapo tarehe 19 Machi 2013, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro na baadaye wakaweza kubadilishana mawazo kidogo kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.


Rais Napolitano amempongeza Baba Mtakatifu kwa kuchagua jina la Mtakatifu Francisko wa Assisi ambalo lina mvuto na mguso mkubwa katika maisha na shughuli za kichungaji, hali inayojionesha kwa sasa kutokana na ushiriki mkubwa wa waamini na watu wenye mapenzi mema kutoka ndani na nje ya Italia, wanaomiminika kuhudhuria katekesi yake kila jumatano, Sala ya Malaika wa Bwana kila Jumapili na katika Ibada mbali mbali ambazo amekuwa akiziendesha kama Askofu wa Roma.


Rais Napolitano anatambua na kukiri jitihada za Baba Mtakatifu Francisko katika mapambano dhidi ya umaskini miongoni mwa watu wake; jitihada za kulinda na kudumisha misingi ya haki na amani; kutetea zawadi ya maisha na hali tete kwa familia na wakimbizi, wanaodhulumiwa kutokana na ubinafsi na kwamba, Kanisa na Jamii kwa ujumla inachangamotishwa kuwahudumia kwa ukarimu, upendo na mshikamano wa dhati.


Waitaliani ambao kwa miaka mingi walijihesabu kuwa ni sehemu ya “nchi matajiri”, lakini leo hii kuna mamillioni ya wananchi wanakabiliana na umaskini na hali ngumu ya maisha kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa ambao umeonesha makucha yake kwa takribani kipindi cha miaka kumi sasa. Kuna idadi kubwa ya watu hasa vijana wasiokuwa na fursa za ajira, jambo linalohitaji anasema Rais Napolitano kufanya tafakari ya kina, kuwa na mwono mpya; kujenga misingi ya haki na mshikamano na kuwasaidia waathirika wa myumbo wa uchumi kimataifa.


Ni changamoto ya kuwa na mwelekeo mpya wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii Barani Ulaya, kwa kutambua na kufanyia kazi changamoto zinazojitokeza kwa nyakati hizi, bila kusahau kuunga mkono jitihada zinazofanywa na nchi changa duniani katika kujikwamua na hali duni ya uchumi. Lakini mabo yote haya hayana budi kuzingatia misingi ya maisha ya kiroho na kimaadili, bila kupoteza dira na matumaini.


Rais Napolitano amelipongeza Kanisa kwa mchango wake wa hali na mali katika maendeleo na ustawi wa wananchi wa Italia, wanapotekeleza utume na dhamana yao katika shughuli mbali mbali za kichungaji. Serikali ya Italia itaendelea kushirikiana kwa hali na mali na Vatican kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watu, haki na amani sanjari na kusimama kidete kutetea uhuru wa kuabudu; majadiliano ya kidini na kiekumene kwa ajili ya mafao ya wengi.


Rais Giorgio Napolitano wa Italia amemshukuru na kumpongeza Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kwa mchango wake makini katika maisha na ustawi wa Kanisa kwa ujumla.








All the contents on this site are copyrighted ©.