Kheri nane za Mlimani
ni muhtasari wa Mafundisho makuu ya Yesu!
Waamini wanaalikwa
kuliishi kikamilifu Fumbo la Ukombozi kwa kutafuta faraja kutoka kwa Roho Mtakatifu
bila ya kuchanganya mambo. Heri nane zilizotangazwa na Yesu ni muhtasari wa Mafundisho
yake makuu kwa wanafunzi wake. Anawataka kwa namna ya pekee wawe na huzuni na umaskini
wa roho; wawe na njaa na kiu ya haki; wawe na rehema, wenye moyo safi na wapatanishi.
Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko
wakati wa Ibada ya Misa Takatifu, Jumatatu tarehe 10 Juni 2013 kwenye Kikanisa cha
Domus Sanctae Marthae, kilichoko hapa mjini Vatican. Anasema, kheri nane ndiyo faraja
ya Roho Mtakatifu kwa wale ambao wamekombolewa na kuweka mioyo yao wazi kwa ajili
ya kupokea neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kiasi kwamba, wako huru.
Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumwomba Kristo neema ya kuweza
kumfuasa kwa ukamilifu, ikiwa kama wana moyo wazi pamoja na kumwachia nafasi Roho
Mtakatifu ili aweze kuwaletea mabadiliko ya ndani na faraja ya kweli inayowafanya
kuwa huru kiasi cha kutambua na kumwilisha Mafundisho makuu ya Yesu katika uhalisia
wa maisha.