2013-06-07 08:16:37

Mapadre changamkieni utakatifu wa maisha


Askofu mkuu Paul Ruzoka wa Jimbo kuu la Tabora, Tanzania anasema, Maadhimisho ya Mafumbo ya Imani yawasaidie waamini kuchuchumilia utakatifu wa maisha, kwani huu ndio wito wa kwanza kabisa kwa kila mwamini. Wanaalikwa kuwa watakatifu kama Baba yao wa mbinguni alivyo mtakatifu. RealAudioMP3

Utakatifu ni dhamana ya kila Mkristo mbatizwa ambayo kwa njia ya Mlango wa Imani, ameondolewa dhambi ya asili na hivyo kupatiwa neema ya utakaso inayomwezesha mwamini kuliendea Fumbo la Utatu Mtakatifu, chemchemi ya utakatifu wote.

Askofu mkuu Paul Ruzoka anasema kwamba, Mapadre wamepewa dhamana ya kuwaongoza waamini katika hija ya utakatifu wa maisha. Lakini, anawakumbusha Makleri kutambua kwamba, wao wamepewa neema hii kwanza kabisa kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo na baadaye katika Sakramenti ya Daraja Takatifu. Hivyo, kuna umuhimu wa pekee kabisa kwa Makleri kuchuchumilia utakatifu wa maisha unaojionesha katika maisha na utume wao.

Utakatifu wa maisha ni changamoto inayotolewa na Mama Kanisa wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Makleri wawaonjeshe waamini na watu wenye mapenzi mema, harufu ya utakatifu na kwamba, waamini wajitahidi kumwilisha imani kwa njia ya matendo adili, kielelezo cha utakatifu wa maisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.