2013-06-06 09:14:07

Wanaotaka kubinafsisha gesi asilia Mtwara wamtibua tena Kikwete!


Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania amesisitiza kuwa pamoja na kweli kwamba gesi asilia imegundulika mkoani Mtwara lakini gesi hiyo siyo mali ya Wana-Mtwara bali ni raslimali ya Watanzania wote ambao wataitumia kwa manufaa ya nchi nzima. Hata hivyo, Rais Kikwete amesema kuwa wananchi wa Mtwara wanayo haki ya kunufaika na gesi hiyo asilia kama walivyo Watanzania wengine
katika sehemu zote za nchi.

Rais Kikwete ameyasema hayo Jumapili Juni 2, 2013, wakati alipokutana na kuzungumza na Jumuiya ya Watanzania wanaoishi katika Japan kwenye Hoteli ya Royal Park Yokohama mjini Yokohama. Rais Kikwete alikuwa katika ziara ya wiki moja nchini Japan ambako alihudhuria Mkutano wa Tano wa Kimataifa wa Tokyo Kuhusu Maendeleo ya Afrika – TICAD V (Tokyo International Conference on African Development).

Akizungumza na Watanzania hao, Rais Kikwete amesisitiza kuwa raslimali yoyote inayogundulika katika sehemu yoyote ya Tanzania ni mali ya Watanzania wote na lazima itumike kuwanufaisha wote na siyo wale ambako raslimali hiyo imepatikana.

Katika risala yao, Watanzania walikuwa wameeleza kutofurahishwa kwao na ghasia na fujo ambazo zimekuwa zinafanywa Mtwara na baadhi ya watu wanaojiita wakazi wa Mkoa huo wakidai kuwa gesi asilia hiyo ni lazima itumike kuwanufaisha wananchi na Mtwara badala ya kuisafirisha kwenda Dar Es Salaam kuzalisha umeme kwa ajili ya nchi nzima.

Rais amesisitiza kuwa ni jambo lisilokubalika kuwa raslimali ya nchi inaweza kuzuiliwa isitoke katika eneo ambako inapatikana kwa vile hakuna nchi yoyote duniani inayoruhusu jambo la namna hiyo. “Hiyo nchi haipo duniani na wala sera za namna hiyo haziwezi kuanzia Mtwara. Sijui hii dhana wamepata wapi. Nadhani wanavurugwa na wanasiasa ambao wanajitafutia umaarufu. Mafuta ya Texas pale Marekani ni ya Wamarekani wote siyo ya watu wa Texas. Mafuta ya North Sea pale Uingereza ni ya Uingereza yote,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:

“Pato letu la taifa linachangiwa na kila raslimali yetu – migebuka ya Kigoma inachangia, sato wa Mwanza wanachangia, almasi ya Mwadui, dhahabu, pamba na kahawa vyote kwa pamoja vinachangia pato letu la taifa ambalo tunaligawana kwa maendeleo ya kila mmoja wetu. Kule Mtwara kuna mengi yamefanyika kwa nini mbona wana-Mtwara hawajiulizi pesa ya kuyafanya hayo ilitoka wapi? Mbona hawadai kuwa hata korosho isitoke Mtwara?”

Rais Kikwete amekumbusha kuwa siyo mafuta yote yatakayosafirishwa nje ya Mtwara. “Kama nilivyosema ni asilimia 14 tu ya mafuta ambayo itasafirishwa nje ya Mtwara. Asilimia kubwa itabakia Mtwara. Kuna viwanda vingi kiasi cha 47 vitajengwa Mtwara vingi kuliko vilivyo katika eneo lolote la nchi yetu. Linalosubiriwa ni kukamilika kwa upimaji mkubwa wa Mji wa Mtwara na maeneo ya jirani.”

Amesema kuwa ni jambo la kushangaza kuwa wana-Mtwara wanadai kuwa gesi asilia isitoke Mtwara. “Sasa gesi isipokwenda sokoni wana-Mtwara watanufaika vipi? Gesi asilia hii ni lazima iuzwe ili fedha ziweze kupatikana na kuwanufaisha wana-Mtwara na Watanzania wengine.” Rais Kikwete amesema ni jambo la kushangaza vile vile kuwa watu wanaandamana leo kuhusiana na mapato ya gesi. “Mapato ya gesi hii hayataanza kuonekana kati ya miaka sita hadi 10 kuanzia sasa, sasa tunatoana macho ya nini wakati uwekezaji ndio kwanza umeanza?”

Rais Kikwete ambaye aliandamana na mawaziri kwenye mkutano huo na
Watanzania aliwataka mawaziri hao mmoja mmoja kuelezea maswali na
maoni ya Watanzania hao kuhusu maeneo yao. Mawaziri hao ni Waziri wa Uchukuzi Dr. Harrison Mwakyembe, Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo na Waziri wa Kazi na Ajira Gaudensia Kabaka.








All the contents on this site are copyrighted ©.