Utapiamlo ni kikwazo cha elimu kwa watoto wengi wanaotoka katika nchi changa zaidi
duniani!
Shirika la Kimataifa Lisilo la Kiserikali la "Save the Children" linasema kwamba,
ukosefu wa lishe bora miongoni mwa watoto wanaotoka katika nchi zinazoendelea zaidi
duniani ni kikwazo kikubwa katika mchakato wa kuhakikisha kwamba, kunakuwepo na ufanisi
bora wa masomo darasani na kwa kiasi kikubwa ni chanzo cha vifo kutokana na utapiamlo.
Shirika hili linaiomba Jumuiya ya Kimataifa kuwekeza zaidi katika jitihada
za kufanikisha upatikanaji wa lishe bora kwa watoto wanaotoka katika nchi changa zaidi
duniani, ili kuokoa maisha yao pamoja na kuwapatia fursa ya kujiendeleza zaidi kwa
njia ya elimu, kwani elimu kimsingi ni mkombozi wa wengi. Watoto wenye utapiamlo mkali
wanakabiliwa na matatizo mengi ya afya pamoja na kushindwa kukua vyema na hata kushindwa
kusoma. Matokeo yake ni kwamba, utapiamlo unakuwa ni mwendelezo wa umaskini, ujinga
na maradhi.