2013-06-05 08:02:02

Utajiri unaofumbatwa katika Sinodi za Maaskofu Kimabara


Idara ya uchapaji ya Vatican (LEV) hivi karibuni imechapisha kazi kubwa ya ushauri uliotolewa na Mababa wa Sinodi za Kimabara na kuhaririwa na Askofu mkuu Nikola Eterovic, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu kwa kutambua kwamba, Mama Kanisa yupo kwa ajili ya Kuinjilisha na kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia kwa watu wa nyakati zote. RealAudioMP3

Kitabu hiki ni matunda ya kazi ya ushauri uliotolewa na Mababa wa Sinodi za Maaskofu kuanzia mwaka 2004 hadi mwaka 2012. Kwa maneno mengine, hizi ni Sinodi ambazo zimesimamiwa kwa namna ya pekee na Askofu mkuu Nikola Etrovic tangu alipopewa dhamana hii na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili.

Huu ni utajiri wa maisha na utume wa Kanisa mahalia kutoka sehemu mbali mbali za dunia; unaoonesha umoja na mshikamano na Khalifa wa Mtakatifu Petro katika utekelezaji wa shughuli na mikakati ya kiuchungaji kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la kiulimwengu. Umuhimu na haja ya Uinjilishaji Mpya ni changamoto iliyotolewa kwa namna ya pekee kabisa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican miaka 50 iliyopita.

Mapapa waliofuata walianza kuweka mikakati ya shughuli za kichungaji ili kubainisha mbinu ambazo Kanisa lingeweza kutumia katika kutekeleza wajibu huu msingi ambao Kristo mwenyewe ameliachia Kanisa lake. Maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu imekuwa ni fursa kwa Mama Kanisa kuweza kusali, kutafakari na kushirikishana uzoefu, mang’amuzi na vipaumbele kutoka kwa Makanisa mahalia.

Bado Kanisa linatumwa kutangaza Habari Njema kwa watu ambao hawajapata fursa ya kusikia Injili ya Kristo, lakini pia Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo linaendelea kuchangamotishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili kufanya Uinjilishaji Mpya kwa kusoma alama za nyakati pamoja na kuwasaidia wale ambao kutokana na sababu mbali mbali wamelegea katika imani na maisha ya Kikristo, ili waweze kuuona tena Mlango wa Imani ambao ni Kristo ambaye ni njia, ukweli na uzima na kuishi mintarafu Mafundisho na Kweli za Kiinjili.

Hadi sasa kuna Sinodi kumi na mbili ambazo zimekwisha adhimishwa hapa mjini Vatican kwa ajili ya Makanisa mahalia na baadaye kufuatiwa na Nyaraka za Kichungaji kutoka kwa Mababa Watakatifu. Washauri wa Sinodi za Maaskofu wana nafasi maalum katika Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu: Wao wanafanya maandalizi ya kina katika Maadhimisho ya Sinodi kwa kuandaa hati elekezi inayojulikana kwa lugha ya Kilatini kama “Lineamenta” inafuatiwa na hati ya kutendea kazi “Instrumentum Laboris” ambayo kimsingi ni mkusanyiko wa mawazo mbali mbali yanayogusa masuala ya kichungaji, kitaalimungu na kikanisa.

Kitabu hiki ambacho kina utajiri mkubwa, kinaonesha hotuba zilizotolewa na Askofu mkuu Nikola Etrovic wakati wa maadhimisho ya Sinodi hizi. Kuna hotuba za Papa Yohane Paulo wa Pili na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita. Sinodi za Maaskofu zimekuwa ni nyenzo muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa. Zimesaidia kuvumbua utajiri wa historia, maisha na utume wa Kanisa Katoliki kutoka kila pembe ya dunia, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya anasema Askofu mkuu Nikola Etrovic.








All the contents on this site are copyrighted ©.