2013-06-04 09:08:26

Masista watatu wa Shirika la Misericordia, Dodoma waweka nadhiri za kwanza!


Kwa njia ya nadhiri ya usafi kamili, ufukara na utii, maisha ya kitawa yanakuwa ni ushuhuda wa kinabii kati ya watu wanaowazunguka na kikolezo kikubwa cha haki, amani, upendo na upatanisho. Maisha ya kitawa ni ushuhuda wa upendo wa Kristo kwa Kanisa lake, unaoimarishwa kila siku kwa Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, Sala za Kanisa na Utume kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Mama Kanisa anaendelea kuwachangamotisha watawa kuishi kwa uaminifu karama na utume wao ndani ya Kanisa mintarafu miongozo ya waanzilishi wao, kwa njia hii wataendelea kulipamba Kanisa kwa karama na mapaji waliyokirimiwa na Roho Mtakatifu daima wakijitahidi kusoma alama za nyakati na kuendelea kushikamana na Maaskofu mahalia katika maisha na utume wa Kanisa. Nadhiri zinawawezesha watawa kujitoa kwa ajili ya Mungu na jirani zao, huku wakiendelea kujenga na kuimarisha ufalme wa Mungu kati ya watu wake.

Ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma wakati wa Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Masista watatu wa Shirika la Masista wa Huruma wa Verona (Misericordia) walipokuwa wanaweka nadhiri zao za kwanza, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo Katoliki Dodoma.

Askofu Nyaisonga anasema, ubatizo ni mlango wa imani, unaomwezesha mwamini kushiriki katika mafumbo na maisha ya Kanisa, daima akijitahidi kutekeleza mapenzi ya Mungu kadiri ya wito wake. Nadhiri za kitawa ni kifungo kinachomwimarisha mtawa kuacha yote kwa ajili ya kumtumikia Mungu na jirani, jambo ambalo linapaswa kufanywa kwa hiyari pasi na shuruti.

Kwa njia ya Nadhiri za kitawa, watawa wanaweka pembeni haki nyingine za maisha ya kijamii kama vile haki ya kuwa na mchumba, kumiliki mali na kuamua kadiri ya mapenzi binafsi, ili kujifunga na Mwenyezi Mungu, ili kutumia nguvu na mapaji yao kwa ajili ya sifa na utaswi wa Familia ya Mungu inayowazunguka. Hii ni huduma ya upendo inayopaswa kutolewa pasi na upendeleo. Ni mwaliko wakuwa watii kwa Kristo, Kanisa na Viongozi halali wa Shirika, huku wakijitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Shirika lao.

Wakiishi vyema nadhiri zao, anasema Askofu Nyaisonga watakuwa kwa hakika "wamempiga bao shetani". Amewakumbusha watawa walioweka nadhiri zao za kwanza kwamba, kama binadamu watakumbana na vishawishi lakini wanapaswa kusimama kidete kupambana kufa na kupona kwa kutumia silaha na nyenzo zilizowekwa mbele yao na Mama Kanisa. Kwa kufanya hivi, watawa hawa watakuwa wepesi katika kutenda, wenye hekima na busara. Wajitahidi kutekeleza majukumu yao kwa busara, juhudi na maarifa na kamwe wasilegee katika maisha yao ya kitawa.

Watawa walioweka nadhiri zao za kwanza ni: Sr. Bridgita Clod, Sr. Delphina Raphael pamoja na Sr. Cecilia Marko. Ibada hii imehudhuriwa pia na Askofu mstaafu Mathias Josefu Isuja wa Jimbo Katoliki Dodoma.







All the contents on this site are copyrighted ©.