Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) limesema kuwa litaisaidia Tanzania
katika kuanzisha Benki ya Kilimo nchini kama namna bora zaidi ya kusaidia kuboresha
kilimo na kuwainua wakulima wa Tanzania. Aidha, FAO limesema kuwa litaendelea kuunga
mno jithada kubwa zinazofanywa kwa sasa na Serikali katika kuboresha kilimo na kuwainua
wakulima wa Tanzania kutoka kwenye umasikini.
Msimamo huo wa FAO umeelezwa
na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Mheshimiwa Dr. Jose Graziano da Silva wakati alipokutana
na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya
Mrisho Kikwete kwenye hoteli ya Intercontinental mjini Yokohama, Japan.
Mkurugenzi
Mkuu huyo ametoa ahadi hiyo ya FAO kusaidia katika uanzishwaji wa Benki ya Kilimo
Tanzania baada ya kuelezwa na Rais Kikwete kuhusu mipango ya Serikali ya Tanzania
kuanzisha Benki hiyo kama namna ya uhakika zaidi ya uwezeshaji wa sekta ya kilimo
na wakulima nchini.
Dr. Jose Graziano da Silva amemwambia Rais Kikwete: “Hili
ni jambo zuri sana, nilikuwa sijapata nafasi nzuri ya kujua mipango hii. Ahadi yangu
ni kwamba FAO itawasiliana haraka iwezekanavyo na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa
(UN) ili kuangalia namna gani ya kusaidia uanzishwaji wa Benki. Ninachoweza kukuhakikishia
Mheshimiwa Rais kuwa na sisi tutasaidia jitihada za Serikali yako kuanzisha Benki
hii ambalo ni wazo zuri,” amesema Mkurugenzi mkuu huyo na kuongeza:
“Jitihada
za Serikali yako ya kutoa ruzuku kwa wakulima ambazo mmekuwa mnazifanya ni jitihada
nzuri sana na zimechangia katika kuinua uzalishaji na mapato ya kilimo. Hata hivyo,
ruzuku ina mipaka yake kwa sababu haiwezi kutolewa wakati wote na kwa kila mkulima.
Jibu sahihi ni kuwa na Benki ya Kilimo ambayo itatoa mikopo nafuu kwa wakulima.”
Mkurugenzi
huyo wa FAO pia amemwalika Rais Kikwete kushiriki katika shughuli mbili kubwa za FAO
ukiwamo Mkutano Mkuu wa mwaka wa Shirika hilo ambao umepangwa kufanyika makao makuu
ya FAO mjini Rome, Italia kati ya Juni 15 hadi 22 mwaka huu. Mkurugenzi huyo pia amemwalika
Rais Kikwete kushiriki katika Mkutano Maalum wa Kuanzisha Kampeni ya Kutokomeza Njaa
Duniani ifikapo mwaka 2025.
Mkutano huo umepangwa kufanyika mjini Addis Ababa,
Ethiopia Julai Mosi, mwaka huu, 2013 na Kampeni hiyo imebuniwa na Rais Mstaafu wa
Brazil, Mheshimiwa Lula Silva. Rais Kikwete amekubali mialiko hiyo na akasema kuwa
Serikali itaangalia nani ataweza kuiwakilisha Tanzania katika mikutano hiyo muhimu.