2013-06-03 07:11:44

Watanzania wanahimizwa kutunza mazingira, vyanzo ya maji, usafi na ujenzi wa vyoo bora!


Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema Tanzania inapoteza kiasi cha hekta 400,000 za misitu kila mwaka kwa sababu ya ukataji miti unaochochewa na matumizi ya kuni, mkaa, mbao, ujenzi ama uchomaji moto misitu.

Alikuwa akizungumza na mamia ya wakazi wa mji mdogo wa Namanyere, wilayani Nkasi mkoani Rukwa wakati akizindua Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyoanza Jumamosi, Juni Mosi, 2013 ambayo Kitaifa yanafanyika mkoani Rukwa. Maadhimisho hayo yatahitimishwa Juni 5, mwaka huu.

Alisema utafiti uliofanywa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (Tanzania Forest Services - TFS) chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mradi wake wa Tathmini ya Rasilimali za Misitu Nchi unaonesha kuwa ukataji huo wa misitu unasababishwa kuzalishwa kwa tani milioni moja za mkaa ambao nusu yake unatumiwa na wakazi wa Jiji la Dar es Salaam.

“Tanzania inakadiriwa kuzalisha kiasi cha tani milioni moja za mkaa kila mwaka, nusu yake yaani tani 500,000 zinatumika Dar es Salaam peke yake. Kuni zinatumika sana vijijini wakati mkaa unatumika sana mijini. Ndiyo sababu tunasisitiza kwamba, kama tukiwapatia wakazi wa mijini hususan wale wa Dar es Salaam nishati mbadala kama vile gesi, umeme na nishati itokanayo na jua, tutakuwa tumepunguza kwa kiasi kikubwa ukataji miti nchini kwa ajili ya kutengeneza mkaa,” alisema.

Aliwasihi wakazi wa Nkasi na mkoa wa Rukwa kuhakikisha wanajenga nyumba bora zenye vyoo bora kwani ni njia ya uhakika ya kutunza usafi wa mazingira na kupunguza maradhi ya kuambukiza.

“Watu wamezoea kujenga nyumba nzuri lakini hawaweki uzito kwenye suala la choo bora...utakuta choo kidogo tena urefu wake unaishia kifuani tu, unaweza hata kumpungia mtu mkono. Jenga nyumba nzuri na hakikisha unaweka choo kizuri, chooni lazima pawe ni mahali pasafi na pa heshima,” alisisitiza.

Alisema kila Halmashauri hapa nchini inapaswa kulisimamia suala hilo kwani litasaidia kuondoa magonjwa kwa wananchi wake. Alisisitiza utunzaji wa vyanzo vya maji, upunguzaji wa idadi ya mifugo na kuanzishwa kwa ufugaji wa nyuki kama njia ya uhakika ya uhifadhi wa misitu na utunzaji wa mazingira.

“Mkuu wenu wa mkoa kaeleza hapa idadi kubwa ya mifugo iliyomo mkoani mwenu. Suala hapa si wingi wa mifugo mliyonayo bali eneo linalohitajika kwa ajili ya kulishia mifugo. Fugeni kisasa kwa kuzingatia idadi ya mifugo inayotakiwa kwa eneo husika,” alisema.

Mapema akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na wananchi waliohudhuria maadhimisho hayo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano) Bi. Samia Suluhu Hassan aliwataka wakazi hao watunze mazingira, watunze misitu na wasiharibu vyanzo vya maji.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhandisi Stella Manyanya akitoa salamu za mkoa huo kwenye uzinduzi huo alisema uharibifu wa mazingira katika mkoa huo umesababisha kushuka kwa kina cha maji kwenye Ziwa Tanganyika pamoja na Ziwa Rukwa.

“Misitu kwenye mkoa wetu imepungua kutokana na uharibifu wa mazingira. Pia kuna uharibifu wa mazingira unaoendelea kutokana na uzalishaji mkubwa wa taka ngumu pamoja na utupaji hovyo wa takataka... tuache uharibifu huu na tuhifadhi mazingira yetu,” alisisitiza.









All the contents on this site are copyrighted ©.