2013-06-01 08:14:12

Watoto wagonjwa wana mwomba Papa kusali kwa ajili ya watoto wenzao ambao wanateseka kwa magonjwa sehemu mbali mbali za dunia!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa jioni, tarehe 31 Mei 2013, amekutana na kuzungumza na watoto ishirini ambao ni wagonjwa wa saratani kutoka Kitengo cha Watoto, Hospitali ya Agostino Gemelli iliyoko mjini Roma waliosindikizwa na wazazi, madaktari, wauguzi pamoja na viongozi wao wa kiroho, kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican.

Watoto hawa wakati wa hija yao kwenda kwenye madhabahu ya Bikira Maria wa Lourdes walikuwa wamemtumia salam za matashi mema wakimwomba aje kusali pamoja nao!

Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, mkutano kati ya Baba Mtakatifu na watoto hao wagonjwa umefanyika katika hali ya ibada, furaha na matumaini makubwa. Watoto hao wamemwomba Baba Mtakatifu Francisko kusali kwa ajili ya kuwaombea watoto wagonjwa sehemu mbali mbali za dunia pamoja na kuwabariki wazazi na walezi wao wanaojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuwahudumia.

Baba Mtakatifu amewahakikishia watoto hao kwamba, Yesu anawapenda upeo na kwamba, daima yuko pamoja nao hata katika mahangaiko yao. Baba Mtakatifu amewapatia watoto hao baraka zake za kitume, wote wakiwa wamefurahi kukutana na kuzungumza naye ana kwa ana na wala si kama wanavyomwona kwenye Luninga. Watoto hao wamemwahidia Baba Mtakatifu sala zao katika maisha na utume wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.