Rais Josè Alberto Mujica akutana na Papa Francisko mjini Vatican
Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe Mosi, Juni 2013, amekutana na kuzungumza
na Rais Josè Alberto Mujica Cordano wa Uruguay pamoja na ujumbe, baadaye wamekutana
pia na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican na Askofu mkuu Dominique
Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.
Baba
Mtakatifu na mgeni wake, wamebadilishana mawazo na tafakari kuhusu hali ya kisiasa
na kijamii nchini Uruguay na Ukanda wa Amerika ya Kusini. Kwa pamoja wamekazia umuhimu
wa kudumisha maendeleo endelevu yanayozingatia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili;
kulinda na kutetea haki msingi za binadamu bila kusahau haki na haki jamii. Wamepongeza
mchango unaotolewa na Kanisa Katoliki nchini humo na katika medani za kimataifa lakini
zaidi katika huduma ya elimu na afya.