2013-05-30 08:08:18

Wakatoliki jitokezeni kwa wingi kushiriki katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Ekaristi Takatifu!


Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili aliokuwa anaanza utume wake, aliwaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kutoogopa kumfungulia Yesu Kristo malango ya maisha yao. Askofu mkuu Paul Ruzoka, Mwenyekiti wa Tume ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anasema kwamba, hii ni changamoto endelevu inayopaswa kufanyiwa kazi na waamini wa nyakati zote. RealAudioMP3

Waamini wanapaswa kujitokeza kifua mbele kumshuhudia Kristo kwa njia ya maisha yao, kwani Yesu mwenyewe amewaahidia wafuasi wake kwamba, mara atakapokuwa ameinuliwa juu atawavuta wote kwake.

Askofu mkuu Ruzoka anayasema yote haya wakati huu wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Ekaristi takatifu, Wakatoliki wanapoandamana katika mitaa na viunga vya miji yao wakiwa na Ekaristi Takatifu, ili kuwaonesha watu kwamba, Kristo ni Bwana na Mungu anayefanya hija ya maisha akiandamana na wafuasi wake katika uhalisia wa maisha.

Askofu mkuu Ruzoka anawataka Wakatoliki mahali popote pale walipo kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Ibada ya Maadhimisho ya Siku kuu ya Ekaristi Takatifu pamoja na Maandamano ya Ekaristi Takatifu, wakiwa na imani na matumaini kwamba, hatima ya maisha yao iko mikononi mwa Kristo mwenyewe. Yeye atawalinda. Anawataka waamini pia kuwa macho na watu wenye nia mbaya wanaotaka kuvuruga amani, utulivu na uhuru wa kuabudu, kwa kuwajengea waamini hofu isiyokuwa na msingi.

Askofu mkuu Ruzoka anaitaka Serikali ya Tanzania kuwa macho na vitisho vinavyoashilia kuvunjika kwa misingi ya haki, amani na uhuru wa kuabudu. Kamwe Serikali isiruhusu wala kufumbia macho watu wachache wanaotaka kuvuruga misingi ya amani na utulivu nchini Tanzania. "Leo hii wanawajengea waamini hofu ili wasiende Makanisani, lakini kesho na kesho kutwa watanzania watahofia pia kwenda kazini" matoke yake yanaweza kuwa na athari kubwa katika maisha, maendeleo na ustawi wa Tanzania.









All the contents on this site are copyrighted ©.