2013-05-30 11:27:20

Mchakato wa haki na amani upewe msukumo wa pekee katika maisha na vipaumbele vya Kanisa!


Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani anapenda kuwaalika waamini na watu wpte wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kuwa ni wahudumu na wajenzi wa haki na amani mahali wanapoishi na kufanya kazi, hasa wakati huu Kanisa linapomshukuru Mungu kwa Jubilee ya miaka 25 tangu Mtandao wa Imani na Haki kati ya Afrika na Ulaya ulipozinduliwa rasmi.

Kardinali Turkson ameyasema hayo wakati wa Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika mjini Roma, kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 25 tangu Mtandao huu ulipoanzishwa kunako mwaka 1988. Ni mtandao unaoyashirikisha Mashirika 44 ya kitawa na kazi za kitume yanayotekeleza utume wake Barani Afrika na Ulaya kama sehemu ya mchakato unaopania kuhamasisha uwiano sawa katika uhusiano wa kiuchumi baina ya Afrika na Ulaya, ili wananchi wa Bara la Afrika waweze kufaidika na matunda ya jasho lao.

Mtandao huu unatarajiwa kufanya kilele cha Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 25, Mwezi Novemba 2013 hapa mjini Roma kwa kuadhimisha Mkutano mkuu unaotarajiwa kutoa msukumo na ari mpya ya matumaini miongoni mwa wananchi wa Bara la Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.