2013-05-30 16:02:33

Chuo Kikuu cha Madaba ni jukwaa la majadiliano ya kidini; mahali pa kutafuta ukweli na mafao ya wengi!


Mto Yordani una umuhimu wa pekee katika historia na maisha ya Kikristo. Hapa ni mahali ambapo Yesu alibatizwa na ubatizo ni mlango wa Imani na Maisha ya Kikristo. Ni maneno ya Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Makanisa ya Mashariki wakati wa ufunguzi wa Chuo Kikuu cha Madaba nchini Yordani pamoja na kuwasilisha salam na mateshi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa viongozi na wananchi wa Yordani. Katika salam hizi, Baba Mtakatifu Francisko amewaahidia sala na sadaka yake kwa ajili ya kulinda na kudumisha msingi wa haki na amani huko Mashariki ya Kati.

Baba Mtakatifu anatambua na kuthamini mchango unaoendelea kutolewa na viongozi wa Yordan katika mchakato wa ujenzi wa mshikamano na uelewano wa kimataifa. Anawaombea wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Madaba ambacho kimefunguliwa rasmi Alhamisi, tarehe 30 Mei 2013, tukio ambalo limehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Kanisa na Serikali. Chuo hiki anasema Kardinali Sandri ni matokeo ya sadaka ya Wakristo huko Mashariki ya Kati pamoja na mchango uliotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, tangu Chuo hiki kilipoasisiwa!

Kardinali Sandri anasema, Chuo Kikuu cha Madaba ni kielelezo makini cha vipaumbele vya Kanisa na Serikali katika maboresho ya sekta ya elimu kwa vijana wa kizazi kipya ambao kimsingi ni tumaini la Taifa na Jeuri ya Kanisa. Kwa njia ya elimu makini: umaskini, ujinga, shida pamoja na mahangaiko ya mwanadamu yanaweza kupatiwa ufumbuzi wa kudumu. Elimu hii haina budi kukamilishwa kwa kuzingatia kanuni maadili na utu wema unaopaswa kuundwa kwa njia ya dhamiri nyofu mintarafu imani za vijana husika ili kutafuta mafao ya wengi.

Chuo Kikuu ni jukwaa makini la majadiliano ya kidini miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali nchini Yordani; ni mahali pa kutafuta ukweli na mafao ya wengi huku wananchi wakiheshimiana na kuthaminiana kwa kutambua kwamba, wote ni watoto wa Mwenyezi Mungu, changamoto endelevu kwa Wanajumuiya wa Chuo Kikuu cha Madaba, ili kuponya makovu ya utengano na chuki miongoni mwa Jamii. Kanisa linapenda kuchangia katika mchakato wa maendeleo bila ya kuhatarisha utamaduni na mapokeo ya wananchi husika.







All the contents on this site are copyrighted ©.