2013-05-29 09:40:23

Mshahara wa ufuasi wa Kristo ni Msalaba na Madhulumu!


Mateso na mahangaiko ni kati ya changamoto ambazo Wafuasi wa Kristo wanaalikwa kuzimwilisha katika maisha yao kama kielelezo cha ufuasi wa Kristo bila ya kukata tamaa, Kama ilivyokuwa kwa Kristo mwenyewe, wafuasi wake wataendelea kukabiliana na madhulumu na nyanyaso, lakini watambue kwamba, Kristo ameshinda yote.

Ni sehemu ya mahubiri ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, kilichoko hapa mjini Vatican siku ya Jumanne, tarehe 28 Mei 2013. Baada ya Yesu kuainisha jinsi itakavyokuwa vigumu kwa matajiri kuingia kwenye Ufalme wa Mungu, mitume walishikwa na bumbuwazi na kumuuliza, Je, wao ambao wameacha yote, watapata faida gani? Yesu anawajibu kwa macho makavu kabisa kwamba, watapata yote kwa ziada, lakini pia watakabiliwa na madhulumu, huu ndio utakaokuwa mshahara wao mkubwa zaidi.

Wakristo sehemu mbali mbali za dunia wanaendelea kukabiliana na madhulumu na taabu za maisha, changamoto kwa wafuasi wa Kristo kuibeba vyema Misalaba yao na kumfuasa Kristo aliyejinyenyekesha hata akateswa na kufa Msalabani, kielelezo cha unyenyekevu wa hali ya juu kabisa. Wakristo wanapaswa kujitoa kimaso maso wakitambua kile wanachofanya katika maisha yao.

Kuna baadhi ya watu wenye majina na sifa kemkem ambao walidhani kwamba, kumfuasa Kristo ni kujijengea jina na hatimaye, kupata marupu rupu kibao! Watu wa namna hii anasema Baba Mtakatifu wamemezwa na malimwengu na wanasahau kwamba, mateso na madhulumu yatawaandama katika hija ya maisha yao, kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Petro na mitume wengine.

Baba Mtakatifu anawaalika Wakristo kumshuhudia Kristo kwa maisha na matendo yao, kwa njia ya huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kama alivyofanya Mama Theresa wa Calcutta. Ni Mtawa ambaye alitumia muda wake mwingi kwa ajili ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, humo akajichotea nguvu ya kuwahudumia maskini na wanyonge wa dunia hii kwa upendo wa Kikristo, akithamini utu na heshima yao kama watoto wa Mungu.

Wakristo waguswe na ujumbe wa Neno la Mungu litakalowawezesha kufanya mabadiliko katika maisha sanjari na kuwapatia nguvu ya kuweza kukabiliana na madhulumu katika hija ya maisha yao hapa duniani. Ufuasi wa Kristo unaambatana na upendo wa kweli, hatua kwa hatua. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumwomba Kristo neema na ujasiri wa kutolea ushuhuda amini, kwani Kristo yuko pamoja nao katika shida na magumu ya maisha.

Ibada hii ya Misa takatifu imehudhuriwa na viongozi waandamizi kutoka Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Uinjilishaji Mpya, Wafanyakazi wa kitengo cha umeme na useremala kutoka Sekretarieti ya Vatican.









All the contents on this site are copyrighted ©.