Mkutano wa Maendeleo ya Bara la Afrika waanza nchini Japan
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania ameondoka, Jumanne 28 Mei, 2013 kuelekea Japan
ili kushiriki katika Mkutano wa Tano wa Kuzungumzia Maendeleo ya Afrika ujulikanao
kama Tokyo International Conference on African Development (TICAD - V) uliopangwa
kufanyika mjini Yokohama Juni Mosi hadi 3, mwaka huu, 2013. Rais Kikwete amealikwa
kushiriki katika Mkutano huo na Waziri Mkuu wa Japan Mheshimiwa Shinzo Abe, mkutano
huo pia utaadhimisha miaka 20 tokea kuanzishwa kwa mchakato wa mikutano ya TICAD.
Mkutano
huo – TICAD V utawashirikisha viongozi wa Afrika, viongozi wa Japan na washirika wa
maendeleo ya Afrika ikiwamo Benki ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB),
Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Afrika (AU) na Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa
(UNDP) na utafunguliwa na Waziri Mkuu wa Japan, Mheshimiwa Abe.
Wengine waliopangwa
kuzungumza kwenye sherehe hiyo ya ufunguzi wa Mkutano huo mkubwa ni Waziri Mkuu wa
Ethiopia Mheshimiwa Hailemariam Desalegn ambaye ni Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa
Afrika (AU), Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Mheshimiwa Ban Ki Moon na Mwenyekiti
wa Kamisheni ya Afrika Mheshimiwa Dkt. Nkosazana Dlamini Zuma.
Katika tukio
lake la kwanza kubwa baada ya kuwasili nchini Japan, Rais Kikwete atakutana na kufanya
mazungumzo na Waziri Mkuu Mheshimiwa Abe katika mkutano uliopangwa kufanyika mjini
Tokyo keshokutwa. Mbali na kukutana kwa mazungumzo na Waziri Mkuu, Rais Kikwete pia
atakuwa miongoni mwa kundi la viongozi wa Afrika watakaokutana na Mfalme wa Japan,
H.M. Akihito.
Katika mkutano kati ya viongozi hao wawili, Waziri Mkuu wa Japan
anatarajiwa kuwa atatangaza kuwa Japan inaifutia Tanzania deni la dola za Marekani
milioni 220 likiwa ni deni la mchele ambao Tanzania iliupata kutoka Japan chini ya
mikataba iliyotiwa saini kati ya mwaka 1980 na 1983 kati ya Mamlaka ya Chakula ya
Japan na Serikali ya Tanzania.
Aidha, inatarajiwa kuwa Mheshimiwa Abe atatangaza
rasmi kuwa Japan itagharimia ujenzi wa barabara ya juu kwa juu (fly-over) katika eneo
la Ubungo, Dar es Salaam, kama moja ya hatua za kupunguza msongamano katika jiji hilo.
Mbali na kuungana na viongozi wenzake wa Afrika kuhudhuria mkutano wa TICAD V, Rais
Kikwete pia anatarajiwa kukutana na kuzungumza na wakuu wa mashirika makubwa na kimataifa
ya kibiashara na uchumi ya Japan ambayo yanapenda ama kuimarisha shughuli zake za
uzalishaji ama kuanzisha shughuli mpya katika Tanzania.
Miongoni mwa viongozi
wa mashirika ambayo Rais Kikwete atakutana nayo ni wa Somitomo Corporation ambayo
inashiriki katika kuendeleza miradi ya umeme katika Tanzania, Nitori Holding ambalo
linajaribu kuwekeza katika sekta ya nguo na kilimo cha pamba katika Tanzania na Mitsubishi
Corporation ambalo liko katika shughuli za utafutaji gesi asilia na mafuta.
Mkutano
wa TICAD V miongoni mwa mambo mengine utajadili mchango wa sekta binafsi, biashara
na uwekezaji kama injini za maendeleo, jinsi gani Afrika inavyoweza kuimarisha sekta
ambazo zimejithibitisha kuwa misingi ya kukua kwa uchumi wa Bara la Afrika, Ajenda
ya Maendeleo baada ya mwaka 2015 ambao ni mwisho wa utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo
ya Milenia (MDG’s). Hatimaye, mkutano huo utatoa Azimio ya Yokohama 2013 na Mpango
wa Utekelezaji wa Yokohama kwa miaka 2013 hadi 2017.
Mikutano ya TICAD (TICAD
Policy Forum and Conference) ilianzishwa mwaka 1993 na Japan kwa kushirikiana na UN,
UNDP na Benki ya Dunia kwa njia ya kujadili na kuendeleza ajenda ya maendeleo ya Bara
la Afrika. Chini ya mchakato huo wa TICAD, Japan hujenga mazingira ya kuunga mkono
ajenda ya maendeleo ya Bara la Afrika ambalo nalo ndilo linamiliki na kuongoza jukumu
ya kimsingi la kujiendeleza kwa kushirikiana na Bara la Asia na Jumuia ya Kimataifa.
Tokea ulipofanyika mkutano wa kwanza – TICAD 1 mjini Tokyo Oktoba 5-6, mwaka 1993,
imefanyika mikutano mingine mitatu na kujenga mazingira mazuri zaidi ya jinsi Japan
na Jumuiya ya Kimataifa inavyoweza kuchangia maendeleo ya Afrika.